Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

Wednesday, September 3, 2014

Tambua umuhimu wa tende kwa afya yako



Na Seif Oddo
Tende ni tunda ambalo limethibitishwa kuwa na manufaa makubwa katika mwili wa binadamu endapo litatumika ipasavyo.

Tunda hili ni maarufu katika nchi za mashariki ya kati na sehemu nyingine duniani. Lakini asili ya tunda hili ni kutoka katika nchi za kiarabu na liliingia Afrika Mashariki mnamo karne ya 7.

Nchini Tanzania tende hupatikata kwa wingi kisiwani Zanzibar pamoja na Pemba, ambapo imekua kama ni sehemu ya chakula cha kiutamaduni visiwani humo. Mbali na ladha yake nzuri ya tenda, lakini pia tunda hili limekuwa likitajwa hasa katika vitabu vitukufu vya dini.

Aidha, tunda hili limekuwa likitumiwa sana na waumini wa dini ya Kiislamu hususani katika kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Ambapo Shekhe Khalfan Tiwany wa Chakechake Pemba anaeleza kuwa, tende ni miongoni mwa vyakula vilivyotajwa katika Quraan Tukufu. Huku akiongeza kuwa, katika kisa maarufu cha kuzaliwa Nabii Issa, mama yake Bi. Maryam aliamriwa kula tende baada ya kujifungua, ili kurudisha damu nyingi aliyoipoteza baada ya kujifungua pamoja na kurudisha nguvu ya mwili wake kwa haraka.

Mbali na hayo, wataalam wa tiba wamethibitisha kuwa tende ni chanzo cha virutubisho na nishati mwilini, pia huwezesha kuupatia nguvu mwili kwa haraka sana na hii ndio sababu ya tunda hili kutumika kwa wingi katika Mfungo wa Ramadhani, kwani waumini waliofunga hulitumia tunda hili ili kurudisha nguvu na nishati iliyopotea mchana kutwa walipokuwa wamefunga.


Wataalam wanaendelea kueleza kwamba, ndani ya tende kuna virutubisho kama vile ‘calories,’ ‘calcium,’protein,’ ‘potassium,’ ‘magnessium,’phosphorous,’vitamin A’foliate’ na ‘carbohydrates,’ ambavyo vyote ni muhimu katika miili yetu kiafya.

Hata hivyo, Dk, Ally Khamis wa Hospitali Kuu ya Mnazi mmoja Kisiwani Zanzibar ameeleza kuwa, tende ni chakula cha afya na huwa na mkusanyiko wa ‘vitamin A,’ ambayo husaidia katika kuongeza nuru ya macho, pia kuna madini ya ‘calcium,’ ambayo husaidia kuimarisha mifupa, hali kadhalika ndani ya tunda kuna ‘vitamin B6’ na B12, ambazo husaidia katika usagaji na ufyonzaji mzuri wa chakula na kuingia katika mishipa ya damu.

Hali kadhalika, tunda hili linaelezwa kuwa na uwezo wa kutoa kinga dhidi ya maradhi ya saratani ya tumbo (Colon Cancer). Pia huweza kuimarisha moyo na kuukinga dhidi ya maradhi.

Mbali na hayo, tende pia hutibu maradhi ya tumbo kama vile kujaa gesi, kuharisha na kuchafuka kwa tumbo. Pia wataalam wanaeleza kuwa tende husaidia kuondoa sumu mwilini na kusaidia kuongeza nguvu za kiume endapo litatumika kwa kufuata ushauri wa kitabibu.

Tende ni tunda pekee lenye uwezo wa kuupa mwili vitu vinne kwa wakati mmoja ambavyo ni protini, wanga, vitamin na mafuta. Pia tende ni tunda ambalo huyeyuka haraka sana tumboni, hivyo kutolipatia tumbo shida ya kufanya umeng’enyaji (Digestion).

Sambamba na hayo, wataalam wa afya wanaeleza kuwa, tunda hili husaidia kutanua misuli ya mji wa mimba na hivyo basi humsaidia mwanamke kutopoteza damu nyingi wakati wa kujifungua. Aidha, wataalam wa afya wanaendelea kueleza kwamba tende ni chakula bora kwa wanawake wanaonyonyesha kutokana na kusaidia kuyapa maziwa virutubisho muhimu ambavyo humfanya mtoto kuwa na afya bora.

Mbali na hayo, tende ni chanzo kizuri cha madini ya chuma, ambayo husaidia kuwapa ahueni watu wenye upungufu wa damu mwilini. Hivyo basi mbali na kupenda kutumia tende kipindi cha Mwezi wa Ramadhani tu, ni vizuri tukatumia siku zote kama tunavyotumia vyakula vingine, ili kuweza kuimarisha afya zetu kikamilifu.

Makala kama hizi hupatika katika gazeti la TABIBU ambalo linatoka kila siku ya Alhamis na kupatikana nchi nzima kwa shilingi 500/=


No comments:

Post a Comment