Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

MICHEZO

SIMBA, YANGA KUONESHANA UBABE
DIRISHA DOGO
Na Mwandishi wetu
DIRISHA dogo la usajili kwa timu za Ligi Kuu Bara na zile zinazoshiriki Ligi Daraja la Kwanza litafunguliwa rasmi Novemba 15 wakati timu za Ligi Kuu zikiwa zimecheza mechi saba pekee tofauti na 13 kama ilivyokuwa msimu uliopita.

Dirisha hilo litafunguliwa Desemba 15 ambapo klabu za Yanga na Simba zinatarajiwa kuwa kati ya timu ambazo zitanufaika na usajili huo kutokana na uhitaji mkubwa wa wachezaji wapya kwenye vikosi hivyo.

Simba itasajili kiungo mkabaji wa kusaidiana na Jonas Mkude, mabeki wawili wa pembeni pamoja na straika mmoja ili kuimarisha kikosi hicho ambacho hakijaonja ushindi wowote katika mechi nne za mwanzo msimu huu.

Hata hivyo, dirisha la mwaka huu halitarajiwi kuwa na usajili wa kihistoria kama ilivyotokea kwenye usajili wa dirisha dogo msimu uliopita ambapo Yanga ilifanya usajili wa wachezaji wawili wa zamani wa Simba, Emmanuel Okwi na kipa Juma Kaseja kwa fedha za maana.

Lakini wapo baadhi ya wachezaji ambao dirisha dogo litakuwa na mkosi kwao. 

Wachezaji ambao wanatarajia kufunguliwa milango ya kutokea ni pamoja na Uhuru Seleman, Ivo Mapunda, Pierre Kwizera na Amri Kiemba wa Simba wakati Said Bahanuzi na Hamis Thabiti wa Yanga nao wakiwa shakani. Ismail Diara wa Azam naye huenda akakumbana na panga kwenye dirisha hilo.


Mbeya City nayo huenda ikafanya usajili wa straika mpya kikosini hapo kutokana na safu yao ya ushambuliaji kushindwa kufunga.



C. RONALDO: MAN U ITASHINDA LIGI KUU UINGEREZA
London, England


Mchezaji nyota wa klabu ya Real Madrid, Christiano Ronaldo amebashiri kwamba klabu ya Manchester United maarufu kama ‘Mashetani Wekundu’  itashinda Ligi Kuu ya Uingereza chini ya ukufunzi wa Louis Van Gaal.
Kulingana na gazeti la Mirror nchini Uingereza, mchezaji huyo anaamini kwamba klabu hiyo aliyoichezea miaka ya 2003 hadi 2009 imefanikiwa kupata meneja mwenye uwezo wa kuiweka timu hiyo katika kiwango ilichowekwa na aliyekuwa kocha wake Sir Alex Ferguson.

CR-7 kama anavyojulikana na wengi amesema kuwa japokuwa klabu ya Chelsea chini ya ukufunzi wa Jose Mourinho itamaliza katika nafasi ya kwanza msimu huu, kocha Van Gaal atafufua matumaini ya Manchester United.

“Van Gaal ni kocha mzuri ambaye ataifanya Manchester United kuwa bingwa tena na kama si mwaka huu basi mwaka mmoja kutoka sasa,” alisema Ronaldo.



NAHODHA WA BAFANA BAFANA AUAWA
Johannesburg, Afrika Kusini
Nahodha ambaye pia ni golikipa wa timu ya soka ya Taifa la Afrika Kusini Senzo Meyiwa amefariki dunia baada ya kupigwa risasi na watu wasiojulikana, jeshi la polisi la nchi hiyo limesema.

Tukio hilo limeripotiwa kutokea katika nyumba ya mpenzi wake iliyopo katika mji wa Vosloorus kusini mwa Johannesburg.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 aliichezea klabu ya Orlando Pirates na alicheza mechi nne zilizopita za timu yake ya taifa katika mechi za kufuzu za fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika.

Jumamosi alikuwepo katika tukio la timu yake pindi waliposonga mbele katika nusu fainali ya ligi ya Afrika Kusini.

Katika maelezo yake, jeshi la polisi la Afrika Kusini limesema kwamba Meyiwa ameripotiwa kufariki wakati akiwasili hospitalini.

                     UBAGUZI WA RANGI WALITAFUNA SOKA

Na Juma Diwani
Mshambuliaji wa timu ya Ghana anayeichezea Klabu ya Al Ains, Asamoah Gyan amemshtumu mchezaji wa timu ya Al Hilal, Mihai Pintilii kwa kutoa matamshi ya ubaguzi wa rangi wakati wa mechi ya raundi ya pili ya nusu fainali za Klabu Bingwa barani Asia siku ya Jumanne.

Kisa hicho kilitokea baada ya Gyan kupewa kadi nyekundu baada ya kumchezea visivyo Salem Al-Dawsari ikiwa zimesalia dakika 20 kwa mechi hiyo kukamilika.
Pintilii ambaye ni raia wa Romania, alimkaribia Gyan ili kutoa hasira zake hatua iliyosababisha mvutano kati ya wachezaji kutoka pande zote mbili.

“Pintilii alinitolea matamshi machafu,” alisema nahodha huyo wa timu ya Ghana.
Gyan aliongeza kuwa Pintilii hakuwa na haki ya kutoa matamshi aliyoyatamka.

“Hana haki kuniambia yale aliyoniambia tena aliniambia maneno yalionikasirisha na alichoniambia, unaweza kumuuliza.” alisema Gyan.

Gyan aliweka ujumbe wake katika mtandao wa Twitter hivi karibuni akisema kuwa mchezaji huyo alimtolea matamshi ya ubaguzi.


Sanjari na hilo, ni tukio la hivi karibuni la mshambuliaji wa Liverpool kutoka Italia Mario Balotelli aliyetukanwa kutokana na rangi ya ngozi yake kupitia kwa mtandao wa kijamii wa Twitter.




SIMBA: MECHI 3, DROO 3, POINTI 3, YANGA MAMBO POA

Na Kennedy Chaya, Dar

Klabu ya Simba ya Dar es Salaam msimu huu wa ligi kuu ya Vodacom imeanza kwa kusuasua, jambo ambalo halifurahishi mashabiki wake.

Timu hiyo ambayo imecheza mechi tatu, imetoa sare tatu, hivyo kuwapa pointi 3 hali ambayo katika mechi zote iliyocheza imeonesha soka la kawaida tofauti na mategemeo ya mashabiki wao.

Simba Jumamosi iliyopita ilicheza na Shinyanga United, timu changa iliyopanda daraja msimu huu lakini Wekundu hao walishindwa kufurukuta na hatimaye kulazimishwa sare na timu hiyo hali ambayo mashabiki wengi wa Simba walisikika uwanjani hapo wakilalamika kutoridhika na mwenendo wa timu yao.

Mashabiki hao walionekana kutofurahia ushindi wa droo, na hivyo kuwaomba wachezaji wao kucheza kwa kujituma zaidi uwanjani sambamba na kocha Phiri kuweka mfumo ambao utaiwezesha timu hiyo kupata matokeo mazuri.

Wakati hali ikiwa hivyo kwa upande wa Simba, mahasimu wao timu ya Yanga ikionesha mambo yao kunyooka baada ya kupata ushindi wa pili mfululizo ambapo Jumapili iliyopita iliiadhibu timu ya Ruvu Shooting kwa jumla ya mabao 2-1.

Timu ya Yanga sasa imefikisha pointi sita ikiwa nyuma ya bingwa mtetezi wa ligi hiyo Azam Fc.

Timu za Yanga na Simba msimu huu zinahitaji jitihada zaidi katika kupata matokeo mazuri, kinyume chake wategemee kupata matokeo mabaya kutokana na ligi hiyo mwaka huu kuonesha ushindani wa hali ya juu.


No comments:

Post a Comment