Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

MAKALA


Hii ni Kiboko ya U.T.I sugu

Na  Kennedy Chaya 

UNAPOZUNGUMZIA U.T.I si jambo masikioni mwa watu wengi,lakini ukweli ni kwamba neno hilo ni kifupi cha neno Urinary Tract Infection ikiwa na maana ya maambukizi  katika njia ya mkojo,ambayo husababisha bacteria aitwaye Coli.
Mtu yeyote anaweza kupatwa na U.T.I bila kujali jinsia, rika au umri wake wake. Hata hivyo, kuna makundi ambayo kutokana na sababu za kibailojia na kinga ya mwili kushuka au kuwa ndogo huathiriwa zaidi na tatizo hilo.

Katika makundi hayo, wanawake ndio wamekuwa wakionekana kuathirika zaidi kuliko wanaume na hii ni kutokana na mfumo wao mzima wa mkojo kuwa na urahisi wa kuingiliwa na bacteria hao. 

Kwa kuwa mrija wa mkojo yaani urethra ya mwanamke ni mfupi sana ukilinganisha na mwanaume hivyo bacteria hupata urahisi wa kuingia ndani ya mfumo wa mkojo.

Kwa  maneno mengine ni kwamba sehemu ya mkojo ya mwanamke imekuwa karibu sana sehemu ya haja kubwa na bacteria wa Colli kwa kawaida  makazi yake ni kinyeshi, hivyo wakati wa kujisafisha mwanamke ni rahisi sana kama hakuna umakini  kuweza kuchukua bacteria hao kutoka kwenye njia ya haja kubwa hadi ndogo na hivyo kupelekea  kupata U.T.I

Hata hivyo, takwimu za WHO zinaonesha asilimia 4 hadi 5 Ya wanawake wajawazito hupata maambukizi ya U.T.I.

Aidha, watoto nao ni waathirika wakubwa wa U.T.I kutokana na utegemezi walio nao wakati wa kujisaidia ambao unaweza kuwa ni sababu hatarishi kwa wao kupata tatizo hili, pia inaweza kuwa hatari zaidi kwa watoto hadi kupelekea kifo endapo bacteria hao watasambaa hadi kwenye damu na mwili mzima.

Kwa mujibu wa tafiti za taasisi ya magonjwa nchini Marekani (NKUDIC) iliyopo New York Marekani zinaonesha kuwa takribani watu milioni 8.1 duniani kote hutafuta tiba katika vituo vya afya kutokana na tatizo la U.T.I.

Madaktari wanasemaje kuhusu tatizo hilo?
TABIBU ilizungumza na Dk.Herbet Mngoma kutoka hospitali ya Shree Hindu Manal iliyopo jijini Dar es Salaam ambapo alisema kuwa miongoni mwa sababu zinazopelekea maambukizi ya ugonjwa huo ni pamoja na uchafu wa vyoo,matumizi ya maji machafu wakati wa kujisafisha au kuoga na kufanya ngono isiyo salama.

Sababu nyingine ni kutokuwa na usafi wa nguo hususan za ndani hali kadhalika kutokunywa maji mengi mara kwa mara ambayo humpelekea mtu kupata U.T.I.


Dalili za U.T.I
Dk.Mngoma alisema moja ya dalili za ugonjwa huo ni pamoja na kuhisi kukojoa mara kwa mara, mauivu au hali ya kujisikia  kuchoma choma wakati wa kukojoa, mkojo kuwa na ukungu na mara nyingine hutoa harufu kali, pamoja na maumivu ya tumbo chini ya kitovu au kupata homa.

Dalili nyingine za hatari zaidi ni kukojoa damu, kupatwa na shinikizo la chini la damu,kutetemeka na kuhisi baridi.Hali kadhalika, bakteria hao wanapofika kwenye ubongo kupelekea mgonjwa kupata mtindio wa ubongo.

Madhara yatokanayo na U.T.I isipopata tiba sahihi
·     Inaweza ikasababisha maambukizi makubwa ya figo(pyenephritis) ambayo yanaweza kusababisha uharibifu wa kudumu wa figo na hivyo kutishia maisha.
·     
Kwa wajawazito, inawezekana kuhatarisha maisha ya mama na mtoto aliye tumboni.

Jinsi ya kujikinga na U.T.I
·     Kunywa maji mengi kila siku, hii itachangia kukojoa mara kwa mara ma hivyo kutoruhusu bacteria kujenga makazi kwenye njia ya mkojo.
·     Zingatia kukojoa kila unapohisi kufanya hivyo kwani si vizuri kuzuia mkojo.
·     Ni vizuri kukojoa mara tu umalizapo tendo la kujamiiana,hii husaidia kutoruhusu bacteria kuingia na kujenga makazi kwenye njia ya mkojo.
·     Kufanya ngono salama.
Kwa wanawake
·     Hakikisha unapo maliza kujisafisha sehemu za siri unaanzia sehemu ya kutolea haja ndogo ndipo usafishe sehemu ya haja kubwa.Hii itakuepusha kupata bacteria walio eneo La haja kubwa kuingia njia ya mkojo.
·     
Epuka kutumia pedi zenye kemikali ya kukata harufu, kwani husababisha kuua bacteria rafiki wa ukeni.Kwa kufanya hivyo, utakaribisha bacteria wa U.T.I kuzaliana kwa wingi. Vilevile, Dk.Mngoma alisema kuwa ugonjwa huo unatibika na alizitaja baadhi ya dawa ambazo hutibu tatizo hili kuwa ni amoxicillin, erythromycin n.k. Hata hivyo, daktari alisisitiza kuwa ni vizuri kuzitumia dawa hizo baada ya kufuata ushauri wa madaktari.

Wataalam wa tiba asili asemaje?
Gazeti hili lilimtafuta mtaalam wa tiba asili, Dk. Majaliwa Ibrahimu kutoka katika kituo cha Mkunazi Herbalist Clinic kilichopo Kigogo jjini Dar es salaam. Daktari huyu alisema kuwa dawa ya asilia inayotibu tatizo hilo ipo na inaitwa  UHT-POWDER  ambayo humsaidia mgonjwa kupona kabisa  na  kutomrejea tena  tatizo hilo, alisema.

Kwa mujibu wa mtabibu huyo alisema dawa yake hiyo ya miti shamba imekuwa msada mkubwa kwa UTI sugu  wengi   waliotumia husasani wanawake na watoto walinufaika nayo.

Mtaalam wa tiba asili kutoka uturuki anasemaje?
Aidha,kwa mujibu wa utafiti wa Dk.Oz ambaye ni raia wa uturuki anasema kuwa hakuna sababu ya kwenda kumuona daktari unapohisi dalili za U.T.I, badala yake unaweza ukajitibu mwenyewe  ukiwa nyumbani.

Unachotakiwa kufanya ni kuchukua hamira kiasi cha robo kijiko cha chai changanya na maji safi na salama glasi moja kisha kunywa mchanganyiko huo.

Kwa kufanya hivyo, utasaidia kutengeneza magadi mwilini amabyo huzuia bacteria wengine wa U.T.I kutozaliwa.

Wananchi wanasemaje kuhusu ugonjwa huu
Kati ya watu 20 waliofanya mahojiano maalum na gazeti hili walionekana kuwa na uelewa kuhusu ugonjwa huu,ingawaje wanawake wengi walionekana kukiri kukabiliwa na tatizo hilo.


Pamoja na hayo, waliiomba serikali kupitia wizara ya afya kutoa elimu zaidi juu ya tatizo hili, jambo ambalo litawaongezea uelewa juu ya ugonjwa huu.


Jinsi ya kupika wali wa nazi
KARIBU mpenzi msomaji wa gazeti la TABIBU. Katika safu hii ya mapishi, leo nitawaelekeza jinsi ya kupika wali wa nazi.

Wali ni chakula kinachopendwa sana na watu wa pwani hususani wali wa nazi. Hiki ni chakula kinachopendwa sana na wakubwa na watoto.

Mahitaji
·     Mchele kilo 1
·     Nazi 2 au paketi 2 nazi ya maji
·     Chumvi kijiko 1 cha chakula
·     Maji 1/2 lita
Jinsi ya kuandaa
-      Osha mchele vizuri, chuja mchanga.
-      Bandika sufuria yenye nusu lita ya maji safi.
-      Yakipata moto, weka nazi yako na chumvi kisha koroga hadi yachemke.
-      Kisha tumbukiza mchele wako, funika na hakikisha moto si mkali sana.
-      Subiri kwa dakika 10 kisha ugeuze vizuri wali wako na mara baada ya dakika 20 wali wako utakuwa tayari.

Waweza kula kwa mboga yoyote.
Ukifuata maelekezo hapo juu, wali wako utakuwa mtamu na wakuvutia. Unaweza sindikiza chakula hiki kwa matunda kama embe, ndizi na nanasi.




Fahamu kuhusu ugonjwa wa Kaswende 1

Na Abdallah Juma

Ugonjwa wa kaswende ni ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya ‘Treponema pallidum’.

Ugonjwa huu ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayoongoza kwa kusababisha madhara mengi.

Maambukizi ya kaswende wakati wa ujauzito huleta madhara mengi sana kama vile kujifungua kiumbe ambacho kimeshakufa, mtoto kuathirika na ugonjwa huu wakati wa kuzaliwa, mtoto kupata matatizo wakati wa ukuaji wake, degedege na kuongezeka kwa vifo vya watoto wachanga. 

Ugonjwa wa kaswende huathiri zaidi ya mimba milioni moja duniani kote kila mwaka na kuchangia theluthi mbili ya vifo vya watoto wanaozaliwa wakiwa tayari wameshakufa katika nchi za maeneo ya chini ya Jangwa la Sahara. Asilimia 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende huishia watoto kufariki wakati wa kuzaliwa.

Pia asilimia nyingine 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende husababisha watoto wanaozaliwa na ugonjwa huu kupata matatizo ya ukuaji, degedege na kuongezeka vifo vya watoto kwa asilimia 50.

Kwa mfano, Taasisi ya kudhibiti Ugonjwa wa UKIMWI nchini Tanzania (Tanzania National AIDS Control Programme) au NACP katika ripoti yake ya utafiti uliofanywa chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii nchini ilitangaza kuwa, maambukizi yote ya kaswende wakati wa ujauzito Tanzania bara kati ya mwaka 2003 hadi 2004 yaliongezeka kwa wastani wa asilimia 6.7 kwa ujumla, kuanzia mkoani Kilimanjaro ambako maambukizi yalikuwa ya asilimia 0.4 hadi mkoani Tabora ambako yalikuwa ya asilimia 32.

Magonjwa ya UKIMWI na kaswende mara nyingi huambatana pamoja ambapo pia ugonjwa wa zinaa wa kaswende huongeza uwezekano wa mtu kupata UKIMWI.

Je, ugonjwa wa kaswende huambukizwa kwa njia gani?
Kama tulivyosema awali, kaswende husababishwa na bakteria aina ya Treponema pallidum.
Miongoni mwa njia za ugonjwa huu nipamoja na
·      Kupitia kujamiiana bila kutumia kinga au ngono zembe na mtu aliyeambukizwa kaswende.
·      Mama aliyepata ugonjwa wa kaswende wakati wa ujauzito anaweza kumuambukiza mtoto wake wakati wa ujauzito.
·       Kuambukizwa kupitia michibuko au mipasuko kwenye ngozi wakati wa kujamiiana au wakati mwingine pale mtu anapogusana na mtu mwenye kaswende ikiwa wote wawili wana mipasuko kwenye sehemu mbalimbali za ngozi zao.

Sio rahisi mtu kutambua kama ana michibuko au la kwenye ngozi kwani mingine huwa midogo sana isipokuwa ile inayoweza kuonekana kwa macho, lakini huweza kuwa njia ya maambukizo.

Dalili na viashiria vya tatizo hili
Dalili na viashiria vya ugonjwa wa kaswende hutegemea aina ya ugonjwa wa kaswende wenyewe.
Kuna aina tano za ugonjwa wa kaswende ambazo ni;
§  Ugonjwa wa kaswende wa awali (Primary syphilis)
§  Ugonjwa wa kaswende wa pili (Secondary syphillis)
§  Kaswende iliyojificha (Latent syphilis)

§  Kaswende ya baadaye (Tertiary syphilis. Itaendelea..............


Ndizi na faida zake kiafya

Na Zamda Haroun

Ndizi ni tunda muhimu Afrika Mashariki na katika nchi za joto na hasa katika visiwa vya Caribbean. Mmea wake huitwa mgomba katika nchi za Afrika Mashariki.
Tunda hili ambalo lina asili ya kusini mwa Asia huonekana na rangi nzuri na mara nyingi tumezoea kuliona shambani au maeneo ya sokoni na limeonekana kuwa na faida nyingi kiafya.
Miongoni mwa faida za tunda hili ni pamoja na kuboresha ngozi, hususani maganda yake ambapo yanaaminika kusaidia kuimarisha ngozi pale yanaposagwa vizuri na kuchanganywa na matunda mengine kama parachichi. Mchanganyiko huo kwa pamoja husaidia kulainisha ngozi na kuifanya kuonekana vizuri na yenye kung’aa.
Aidha, ndani ya ndizi kuna vitamin B6 na vitamini C, lakini vitamini B6 ndio hupatikana kwa kiwango kikubwa zaidi ndani ya tunda hilo kuliko vitamini C ambayo ni kidogo.
Hali kadhalika, ndizi husaidi kuongeza idadi ya chembe chembe nyeupe za damu hivyo huweza kumsaidia mtu katika uboreshaji wa kinga mwilini.
Faida nyingine za ndizi ni pamoja na kuongeza nguvu mwilini. Hii ni kwa sababu tunda hilo huwa na sukari ijulikanayo kama ‘glucose,’ ambayo husaidia sana kuongeza nguvu mwilini, ingawaje sukari hiyo huhitajika katika kiasi maalum mwilini.
Pamoja na hayo, ndizi pia huweza kusaidia sana kukukinga na kupata vidonda vya tumbo kutokana na ‘compounds,’ mbalimbali zilizomo ndani ya tunda hilo. ‘Compounds,’ hizo ambazo hupatikana kwenye ndizi hujenga tabaka nene kwenye kuta za tumbo ambazo husaidia tumbo kuzuia kuathirika na tindikali ijulikanayo kama ‘hydrochloric acid’.
Aidha, ndizi zina ‘enzyme’ inayojulikana kama protease inhibitor,’ ambayo huzuia bakteria wasababishao vidonda vya tumbo.

Hizo ni baadhi ya faida chache tu za ndizi, ingawaje zipo nyingi zaidi, lakini kwa leo tuhitimishie hapo. Hakikisha unadumisha kutumia tunda hili mara kwa mara ili uweze kuimarisha afya yako zaidi.





Maajabu ya ‘Good Luck Plant’

Na Dk. Edger Kapagi
Mmea huu hupandwa sana na watu wengi kama maua hapa nchini Tanzania.

Mmea huu una majina mengi katika nchi za Java, Fiji, Malaysia, Indonesia, Samoa, Hawaii, Sumatra na New Guinea, nk.

Jina la kibotania huitwa ‘Cordyline Terminals’ na majina mengine ni ‘cordyline fluctiosa’, ‘ti plant’, Hawaiian good-luck plant’, ‘false palm’, ‘canade indio’, ‘croto’, ‘keulenlilie’ na ‘red tree of kings’. Waingereza huuita ‘goodluck plant’. Mmea huu hukua hadi kufikia kimo cha mita 1 hadi 3 kufuatana na mazingira ya nchi yalivyo.

Mmea huu huwa na rangi ya zambarau au nyekundu kufuatana na mazingira yalivyo.

Aidha, mmea huu hutumika kutibu magonjwa kama damu inayotoka pamoja na mkojo, damu inayotoka kwenye ‘piles’, kuzuia mimba zinazotoka kabla ya wakati wake, homa, pumu, kuumwa kichwa, kubana kifua, maumivu ya mgongo, kuungua na moto, bawasiri, matende, jongo, uvimbe wa ‘scrotum’, mafua, kikohozi, kifaduro, ‘gastritis’, macho kuuma, fizi zinazotoa usaha, uvimbe unaotokana na kuteguka, ‘gingivitis’, meno kuuma, kipara, mzio, maumivu ya tumbo, ‘enteritis bacillary dysentery’, maumivu ya mifupa yanayotokana na baridi yabisi, maumivu ya sikio na koo.

Kinachotumika ni majani mabichi gramu 60 - 90, mizizi iliyokaushwa gramu 30 - 60 na maua yaliyokushwa gramu 9 - 15 kwa kuchemsha pamoja na maji.

Majani yanachanganywa na mafuta ya mbogamboga au mzeituni kwa kutibu vidonda.

Hapa Tanzania, watu wengi hupanda mmea huu kwenye nyumba zao kama maua wakiamini kuwa ni mmea wenye kuleta bahati na kufukuza pepo wabaya, hupanda kwenye varanda au upenuni mwa nyumba.

Nchini Hawaii, watu hutumia mmea kwenye sherehe mbalimbali kama kuleta baraka, utakaso na kufukuza laana nk.
Huko Java, wenyeji hula majani machanga kama mboga.



KUVIMBA KWA TEZI DUME (PROSTATITIS)
Ni ile hali ya tezi dume kuathirika kutokana na vyanzo mbalimbali mfano, bakteria n. Kuathirika kwa hii tezi dume kunaweza sababisha hata utendaji kazi wake kupungua na inapatikana chini ya kibofu cha mkojo. Kazi yake kubwa ni kuzalisha manii kwa ajili ya kurutubisha na kusafirisha mbegu za kiume kutoka kwenye korodani. Tatizo hili linawaathiri wanaume bila kujali rika lakini wanaume kuanzia miaka 50 wameonekana kuathirika zaidi na hili tatizo

Chanzo cha tatizo
Chanzo kikubwa cha ‘prostatitis’ ni kushambuliwa kwa tezi dume na bakteria mbalimbali ambao wanaweza kuwa ni visababishi vya magonjwa mbalimbali ya zinaa; mfano kaswende, kisonono, pangusa n.k au bakteria wanaoshambulia mfumo wa mkojo (UTI) wanaweza kupenya na kuifikia tezi dume na kuishambulia. Vyanzo vingine ni kushuka kwa kinga za mwili na ajali zinazopelekea kuumia katika eneo ambalo tezi dume ipo. Pia kuna mazingira hatarishi yanayopelekea mwanaume kuathirika na hili tatizo;
·      Kama mwanaume alishawahi kuwa na hili tatizo na hakupata matibabu sahihi
·      Kuwa na maambukizi katika kibofu cha mkojo au mrija unaotiririsha mkojo (urethra)
·      Kutokunywa maji mengi
·      Kuwa na wapenzi wengi na kushiriki tendo la ndoa na mpenzi mwenye maambukizi ya magonjwa ya zinaa na VVU/UKIMWI.

Dalili za hili tatizo
·  Maumivu wakati wa kutoa haja ndogo au kuhisi kama mkojo ni wa moto na maumivu wakati wa kufika kileleni
·      Kwenda haja ndogo mara kwa mara
·      Mtiririko wa mkojo kuwa dhaifu
·      Maumivu chini ya kitovu
·      Maumivu ya kiuno na chini ya mgongo
·    Maumivu ya sehemu ambayo ipo katikati ya korodani na sehemu ya kutolea choo kubwa
·      Maumivu ya korodani na uume
·      Mwanaume mwenye tatizo hili anaweza akawa na homa

Madhara endapo matibabu yatachelewa
·      Kusambaa kwa bakteria mbalimbali katika damu (bacteremia)
·      Kuwa na jipu kwenye tezi dume (prostatic abscess)
·      Ugumba kutokana na kuathirika kwa manii, mbegu za kiume
·      Pia tatizo hili linaweza likasababisha kansa ya tezi dume (prostate cancer)


TUSHIRIKIANE KUTOKOMEZA UKIMWI

Na Juma Diwani
Tatizo la UKIMWI si geni masikioni mwa watu kwani huripotiwa mara kwa mara katika vyombo vya habari, tatizo ambalo husababisha vifo bila kujali rangi wala kabila huku likiongeza umaskini, idadi ya mayatima na watoto wa mitaani.

Aidha,kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), inakadiriwa kuwa watu kati ya milioni 1.4 hadi 1.7 walifariki dunia kutokana na tatizo hilo mwaka 2013.

Wengi wetu tumeshashuhudia jinsi ndugu zetu walivyopoteza maisha yao kutokana na ugonjwa huu. Tunaweza kusema hakuna hata familia moja au mtu yeyote kati yetu Watanzania anayeweza kusema kuwa hajaguswa na athari mbaya za UKIMWI na kama yupo basi ni wa kutazamwa kwa mshangao usiopimika.

Wanaokufa kwa UKIMWI ni nguvu kazi ambayo inaondoka duniani huku mchango wao ukiwa bado unahitajika. Tunasema hivyo tukiamini kabisa kuwa wengi wa wanaokufa kwa UKIMWI kwa sasa ni wasomi, vijana na watu wenye nguvu motomoto katika kutenda.

Inatia moyo hasa kuona kuwa, viongozi wa Serikali katika ngazi mbalimbali hadi kitaifa, wameivalia njuga vita dhidi ya UKIMWI na kuweka mikakati mbalimbali kupigana na ugonjwa huu.

Hata hivyo, bado inasikitisha kwani licha ya juhudi hizo zikiwemo za elimu ya mara kwa mara juu ya UKIMWI, bado ugonjwa huu hatari unazidi kushamiri.

Hata hivyo, yapo mambo mengi yatupasayo kufanya ili kuondokana na ugonjwa huu mbaya lakini kubwa zaidi, tukae chini tuulizane kuwa, ‘kwa nini UKIMWI unazidi kushamiri? Sababu hasa ni nini, nasi tunashindwa wapi? Sasa, kila mmoja afanye nini?’

Huku nyumba za kulala wageni zikielezwa kuwa kichocheo cha tatizo hili, mara nyingi nyumba hizi hutumiwa hata na watu wasiofahamiana kwa muda mrefu ambao huchukuana kiholela na kwenda huko kufanya uzinzi katika nyumba hizo.

Wakati huo huo, gesti nyingi zipo pamoja na baa za vinywaji mbalimbali kama bia na pombe za aina nyingi. Hapo ni vema kila mmoja akumbuke na kuzingatia kuwa kwa asilimia kubwa ya uzinzi na ulevi ni marafiki wakubwa na ndiyo maana kila alipo bwana ulevi si rahisi kumkosa bwana uzinzi.

Hivyo, ni rahisi kwa mtu aliyelewa pombe kutamani kufanya mapenzi na mtu yeyote, bila kufikiria kwa makini, hata kama hamjui, bila woga kwa Mungu na bila aibu kwa watu. Huu ni ukweli ulio bayana.

Binadamu ni kiumbe mwenye akili na utashi, na hivyo akili yake ndiyo inayotawala mwili, lakini kama inatokea kuwa vionjo vya mwili ndivyo vinavyotawala akili basi huyo si binadamu tena aliyeumbwa kwa mfano na sura ya Mungu.

Kwa kadiri ya akili ya binadamu akiambiwa kuwa kuna hatari mahali fulani, hujiweka katika tahadhari ili hatari isimpate, lakini cha kushangaza ni katika ugonjwa huu. Ingawa elimu kadha zinatolewa dhidi yake, tunashuhudia namna wengi wetu wanavyoendelea kupuuzia jambo hilo.

Sote tunapaswa kujua kuwa huo ni ugonjwa ambao kwa kweli unadaiwa hauna tiba bali, una kinga ambayo siyo hasa kondom, bali ni utashi wake binadamu wa kujishinda katika kufanya vitendo vya ndoa nje au kabla ya ndoa.

Katika hatari mbalimbali ambazo binadamu hukumbana nazo, mara nyingine huona kimakosa kuwa kitu fulani ni kinga itakayomsaidia, kumbe sivyo.

Tunao ule msemo usemao, ‘kufa kufaana’ hivyo yawezekana kuwa hata katika janga la UKIMWI, kuna kufa kufaana, yaani kuna watu wanaofaidika kutokana na balaa hilo.

Tunapaswa kuwa waangalifu sana katika kupokea ushauri na hata hizo zinazodaiwa kuwa ni kinga za nguvu. Ni lazima tutambue kuwa hapo kuna vitu vya biashara pia, licha ya kudaiwa kuwa ni misaada ya kutuonea huruma sisi wananchi.

Tumesikia kuwa kuna mikoa inayosifika kwa utumiaji wa kondom, lakini bado hatujaambiwa kwamba hiyo mikoa imepunguza vifo vitokanavyo na UKIMWI kwa kiasi kipi.

Wengi wetu tumekuwa tukisikia kwamba wenzetu wa Uganda wamefanikiwa kupunguza kasi ya UKIMWI siyo kwa sababu waligawiwa na kutumia kondom, bali kwa sababu walikubali kubadili tabia zao.

Kanuni yetu iwe ni ile ya wanausalama, kwamba tusimwamini kila mtu na tumtilie mashaka kila mtu. Haifai kusema kuwa mtu huyu ni salama ama sivyo kwa mtazamo wa macho matupu.

Pia, tusijidanganye kwa kuwaamini wanaodai kupimwa na kuonekana salama siku hiyo kwani cheti hicho si cha kudumu.

Yawezekana kuwa aliyekuwa salama juzi, leo anaweza kuwekwa katika kundi la waathirika hivyo, kinachotakiwa ni kuwa imara katika kuilinda miili yetu.


Hatimaye, tunapaswa kufahamu kuwa UKIMWI upo huku ukizidi kutokomeza watu na ni hatari tushirikiane kuutokomeza.

JE, WAJUA MADHARA YA POMBE KWA AFYA YAKO?

Na Seif Oddo
Pombe ni kinywaji ambacho hutumika kama kiburudisho miongoni mwa watu walio wengi duniani kote. Wengine hutumia pombe kwa lengo la kupunguza mawazo na wapo wanaotumia pombe kwa lengo la kuondoa aibu.

Kampuni mbalimbali zinazojishughulisha na uzalishaji wa pombe, zimekuwa zikijiingizia faida kubwa kutokana na bidhaa hizo kuwa na watumiaji wengi duniani kote.

Mbali na kuwa na wapenzi wengi, lakini utumiaji wa bidhaa hii kupita kiasi umekuwa ukileta madhara mbalimbali kwa watumiaji hawa kila kukicha.

Mashirika ya takwimu nchini Uingereza yanaripoti mnamo mwaka 2007, kulikuwa na vifo 8,724 ambavyo vilihusishwa na pombe nchini humo.

Nchini Scotland, shirika la NHS mnamo mwaka 2003 lilitoa makisio ya kwamba, kifo cha kila mtu mmoja kati ya vifo vya watu 20 vilitokana na pombe.

Utafiti uliofanyika mwaka 2009 pia uligundua ya kuwa watu 9,000 walikufa kutokana na magonjwa yaliyohusishwa na matumizi ya pombe.

Kituo cha udhibiti na uzuiaji wa magonjwa nchini Marekani kinaripoti kuwa, kutoka mwaka 2001 hadi kufikia mwaka 2005, kulikuwa na takribani vifo 79,000 vilivyotokana na matumizi ya pombe kupita kiasi.

Kiafya, matumizi ya pombe huleta madhara mbalimbali ndani ya mwili wa binadamu. 

Kwa mfano, ini huathirika vibaya kutokana na matumizi ya pombe kupindukia.

Pia tumbo nalo huathirika kutokana na kuchubuka kwa ngozi laini ya tumbo la chakula na kusababisha vidonda vya tumbo. Mbali na hapo, lakini pia ubongo nao huathirika, baadhi ya chembechembe za ubongo yaani ‘brain cells’ huharibika na kusababisha tatizo la kupoteza kumbukumbu.

Pia pombe huleta madhara katika moyo na mapafu ya binadamu. Kwa wanawake wajawazito, pombe huwasababishia kuharibika kwa mimba na hata kupelekea kujifungua mtoto mwenye mtindio wa ubongo.

Wataalam wa masuala ya afya wanaeleza kuwa, matumizi ya pombe kupita kiasi, husababisha matatizo ya mishipa, upungufu wa damu na matatizo ya kisaikolojia.

Wataalam hawa wanaeleza ya kwamba asilimia tisini ya watu wenye saratani ya tumbo ni watumiaji wa pombe kupita kiasi. Wanaeleza kuwa pombe husababisha ongezeko la mafuta ndani ya damu, lakini pia pombe huleta unene.

Pia pombe husababisha kutetemeka, kuzubaazubaa na hata kupauka kwa mwili.

Ndio maana hata katika vitabu vya baadhi ya dini kama vile dini ya Kiiislamu, pombe imeharamishwa kwa kuzingatia madhara yake kwa binadamu.

Mbali na madhara ya kiafya, pombe huleta mfarakano ndani ya jamii na hata huvuruga na kuondoa amani ndani ya familia. Pia pombe huathiri uchumi wa mtu kwani pombe ikishakuwa sugu ndani ya mwili wa binadamu (chronic), humfanya sehemu kubwa ya pato lake kuishia kwenye kununua pombe.

Ikumbukwe ya kwamba ndani ya pombe kuna kemikali ambazo huwa ni sumu katika mwili wa binadamu.

Inaelezwa ya kwamba pombe pia huleta madhara kama vile upungufu wa nguvu za kiume, kukosa hamu ya tendo la ndoa (loss of libido), kansa ya figo na kufanya figo kushindwa kufanya kazi yaani ‘renal failure’.

Pia pombe husababisha matatizo ya ganzi miguuni na mikononi ambayo kitaalam hujulikana kama ‘peripheral neuropathy’.

Lakini pia pombe huleta utapiamlo hasa kwa wale wanaokunywa sana huku lishe yao ikiwa duni na pia kuleta saratani ya umio yaani ‘oesophagus’.

Madhara ya pombe hayajaishia hapo lakini pia inaelezwa ya kwamba pombe husababisha saratani ya ini, kusinyaa kwa ini na hata saratani ya tumbo sambamba kabisa na vidonda vya tumbo.

Tazama maajabu haya, katika baadhi ya matangazo ya pombe mwishoni huelezwa kabisa kwamba ‘matumizi ya pombe kupita kiasi ni hatari kwa afya yako, tafadhali kunywa kistaarabu’.


Lakini watumiaji hawazingatii haya na hatimaye hunywa kwa kupitiliza na kujizolea matatizo mbalimbali. Epuka matumizi ya pombe kupindukia kwa ajili ya kulinda afya yako.

FAHAMU FAIDA TISA ZA MBEGU YA MABOGA
Na Zamda Haroun kwa msaada wa Mitandao
UNAWEZA kuzidharau mbegu za maboga, lakini ni miongoni mwa mbegu zenye faida kubwa mwilini, zinazoweza kuzuia na kutibu hata magonjwa hatari yaliyoshindikana hospitalini.
Kwa mujibu wa utafiti wa kisayansi uliokwishafanyika, zifuatazo ni faida za kifya mtu anazoweza kuzipata kwa kula mbegu za maboga, zikiwa mbichi ama zilizokaangwa:

Huimarisha moyo, mifupa

Mbegu za maboga (pumkin seeds), zina kiwango kingi cha madini aina ya magnesium ambayo ni muhimu kwa afya ya moyo, uimarishaji mifupa, mishipa ya damu na ufanisi wa utumbo mpana. Magnesium imeonesha uwezo mkubwa wa kuzuia mshituko wa moyo na kiharusi.

Kinga ya mwili

Mbegu za maboga zina kiwango kingi cha madini aina ya zinc, ambayo yana faida nyingi mwilini, zikiwemo uimarishaji wa kinga mwilini, ukuaji wa seli, macho na ngozi ya mwili. Vile vile, zinc huimarisha nguvu za kiume.

Saratani ya kibofu

Kutokana na kuwa na kiwango kingi cha zinc, utafiti umeonesha kuwa mafuta na mbegu zenyewe za maboga huweza kutumika kama dawa ya kutibu saratani ya kibofu.

Kinga ya kisukari

Utafiti umeonesha pia kuwa mbegu za maboga huweza kuimarisha utokaji wa ‘insulin’ mwilini, hivyo kuwa kinga au kuleta ahueni kubwa kwa wagonjwa wa kisukari.

Tiba kwa waliofikia ukomo

Mafuta ya mbegu za maboga hayana madhara, zaidi yana kirutubisho muhimu cha kurekebisha lehemu mwilini, kushusha shinikizo la damu, kuzuia uvimbe, maumivu ya kichwa, maumivu ya viungo vya mwili na vile vile huondoa maumivu mbalimbali yanayowapata wanawake wenye umri mkubwa waliofikia ukomo wa hedhi (menopause).

Ugonjwa wa ini

Mbegu za maboga pia zina kamba lishe na kinga kubwa ya kupambana na magonjwa nyemelezi. Mbali na hayo, mbegu zina virutubisho vinavyotoa kinga dhidi ya magonjwa ya ini na moyo.

Usingizi

Kwa watu wenye matatizo ya usingizi, wanashauriwa kula punje kadhaa pamoja na tunda lolote muda mfupi kabla ya kupanda kitandani. Utafiti umeonesha kuwa mbegu za maboga zina kirutubisho kinachochea uzalishaji wa homoni za usingizi kwa wingi.

Uvimbe

Mbegu za maboga zimeonesha kuwa na virutubisho vingi vyenye uwezo wa kuzuia magonjwa yote ya uvimbe mwilini, yakiwemo ya kuvimba miguu, vidole na hata majipu.

Jinsi ya kula mbegu

Hakikisha unakula mbegu ambazo hazijaoza na zilizosafi ambazo hazijakaa muda mrefu. Kwa usalama zaidi, zioshe kwa maji safi kisha zianike, inapendeza zaidi ukila bila kukaanga, lakini pia ukiamua kula za kukaanga bado utapata faida zake, muhimu usiziunguze wakati wa kukaanga. Kwa kawaida hukaangwa kwa muda usiozidi dakika 10 tu.


UMUHIMU WA PARACHICHI KWA AFYA
Na Zamda Haroun
PARACHICHI ni tunda linaloupatia mwili vitamini C. Tunda hili hupatikana kwa wingi katika mikoa ya Kilimanjaro, Tanga na Mbeya.

Pamoja na umuhimu wake, tunda hili pia limekuwa likitumiwa na wanawake wengi kama urembo kwa kujipaka usoni na kwenye nywele.

Tunda la parachichi lina faida nyingi kiafya, hususan kuukinga mwili dhidi ya kemikali hatari pamoja na kumfanya mtu kuonekana kijana.

Wanasayansi kutoka kutoka Chuo Kikuu cha Michoacana de San Nicolas de Hidalgo cha nchini Mexico wanaeleza kwamba tunda hilo husaidia katika kuukinga mwili dhidi ya kemikali hatari (free radicals). Hivyo, linatoa kinga dhidi ya magonjwa mengi pamoja na kumfanya mtu kuonekana kijana.

Wanasayansi hao wanaeleza kuwa mafuta yanayopatikana katika parachichi yana uwezo wa kupenya hadi ndani ya injini inayotengeneza nishati mwilini inayopatikana katika seli inayojulikana kama ‘mitochondria’.

Kwa mujibu wa wataalamu hao, ‘free radicals’ ni kemikali zinazosababisha magonjwa mengi yakiwemo baadhi ya saratani, kuharibu mishipa ya damu ya ateri ‘arteries’, pamoja na kumfanya mtu kuzeeka haraka.

Wanaeleza kuwa mafuta yanayopatikana katika baadhi ya mboga za majani, matunda na nyanya/ tungule yana uwezo wa kupambana na kemikali hizo hatari lakini mafuta haya hushindwa kuingia ndani ya ‘mitochondria’ ambako ndiko kuna kemikali hizo hatari kwa wingi.
Kwa upande wake, mtafiti Christian Cortes-Rojo kutoka chuo kikuu hicho cha Mexico ambaye ndiye alifanya utafiti huo, anasema, ‘anti–oxidants’ zinazopatikana katika mboga za majani na matunda mengi haziwezi kupenya ndani ya ‘mitochondria’, hivyo kushindwa kudhibiti kemikali hatari ndani ya ‘mitochondria’ hizo.

Hatua hiyo huelezwa kusababisha kemikali hizo hatari kuendelea kushambulia ‘mitochondria’ na kuziharibu na matokeo yake ni kuwa nishati haitolewi tena kutoka kwenye ‘mitochondria’ na seli hushindwa kufanya kazi na kufa.

Matokeo ya utafiti huu yalitolewa katika Kongamano la kila Mwaka la Chama cha Wataalamu wa Mambo ya Bayokemia na Bayolojia ya Viumbe Hai kutoka nchini Marekani (American Society of Biochemistry and Molecular Biology Annual Conference).

Kemikali hizi hatari ni uchafu na zinatolewa na mwili wakati wa kusaga chakula na huweza kutolewa kwa wingi kwa mtu anayevuta sigara, mtu anapokumbana na mionzi na hata wakati kukiwa na uchafuzi wa mazingira.

Kemikali hizi huharibu mpangilio wa protini katika muundo wa vinasaba.

Wanasayansi hao wakati wanafanya utafiti waliweza kuona ya kwamba mafuta ya parachichi yaliwezesha seli za ‘yeast’ kuishi kwa muda mrefu kwenye madini chuma licha ya kuwekewa kiwango kikubwa cha madini hayo ambayo ndiyo hutoa kemikali hizi hatari kwa wingi.

Katika tafiti ambazo ziliwahi kufanyika huko nyuma nchini Mexico, ambayo inaongoza kwa uzalishaji wa parachichi duniani, zilionesha ya kwamba parachichi hupunguza kiwango cha lehemu mwilini na pia hupunguza baadhi ya mafuta yanayohusishwa na ugonjwa wa kisukari.

Mafuta ya parachichi yana virutubisho sawa na mafuta ya ‘olive oil’ yanayohusishwa kwa kusaidia kupunguza lehemu mwilini pamoja na kinga dhidi ya magonjwa mengi sugu kama inavyoonekana kwa watu wanaoishi katika nchi za Mediterania ambao ni watumiaji wazuri wa mafuta haya ya ‘olive’.

Kwa muda mrefu, wanasayansi wamekuwa wakiita parachichi kama mfalme wa matunda kutokana na kuwa na virutubisho vingi kuliko tunda lingine lolote duniani.

Kutokana na umuhimu wa parachichi, kuna haja kwa kila mwanajamii popote alipo kuhakikisha anazingatia somo hili, ikiwamo kulitumia kwa wingi tunda hili kwa manufaa yake.


Pamoja na kila mtu kuhakikisha anatumia tunda hili, ni muhimu pia kwa serikali na hata wakulima kutilia mkazo kilimo cha matunda haya ili kuboresha afya.


MIUJIZA YA LIWA (SANDALWOOD)
Mmea wa liwa unaaminika kuwa asili yake ni India na ndiko unakotumika sana. Wachina nao wamekuwa wakiutumia kwa miaka mingi iliyopita. Jina la kibotania huitwa ‘Santalum album’. Jina la kibiashara la ‘sandalwood’ hutumiwa sana na Wahindi. Pia jina lingine wanalolitumia Wahindi ni ‘Chandan’.

Tanzania, mti huu tunauita ‘Mliwa’ au kwa Kiingereza ‘Sandal wood’.
Liwa si kitu kigeni katika masikio yetu. Kwa kuwa ilikuwepo tangu enzi za mababu zetu. Kwa hiyo liwa ni kitu cha kawaida katika masikio ya watu.
Liwa inatoa mafuta muhimu yaliyo na ‘santaloe’ ambayo ndiyo muhimu kutibu maumivu ya utokaji wa mkojo (dysuria) na maumivu ya ‘bladder’ (cystitis).

Unga wa liwa ukichanganywa na maziwa hutibu kisonono na matatizo ya sehemu za mkojo na sehemu za siri (genitourinary).

Pia hutibu ‘gastric irritability’ ikichanganywa na maji, sukari, asali na maji ya mchele. Hutibu ‘dysentery’, homa inayosababisha kichwa kuuma, magonjwa ya ngozi na liwa pia husaidia katika kipindi cha joto ambapo watu wengi huharibika nyuso zao kwa vipele pamoja na kubadilika kuwa rangi ya kufifia kwa ajili ya jua kali.

Liwa hutumiwa zaidi na wanawake wa Tanzania visiwani katika kuwapamba maharusi wanapoolewa. Pia hutumiwa na wasichana wadogo waliofika umri wa kuanza kujitegemea.

Matumizi ya liwa hayana madhara yoyote katika mwili wa binadamu. Liwa hutumiwa na wanawake wengi katika kuondoa vipele (chunusi) usoni na pia hukufanya kuwa mng’avu bila kudhuru ngozi yako ya uso au mwili.

Matumizi ya liwa ni rahisi kwa akina mama kwa kuwa haina masharti mengi katika kuandaa na haina kipimo katika kutumia na ina gharama ya chini kuliko vipodozi vingine.

Baada ya kupaka, liwa unashauriwa kutopaka vitu vingine usoni, ikiwemo poda na krimu kwa kuwa ukipaka vitu hivyo wakati wa usiku, vitundu vya ngozi huziba na kushindwa kuingiza hewa vizuri mwilini na kusababisha ngozi kusinyaa kwa kukosa hewa.

Liwa inapakwa mwili mzima lakini hasa usoni ambapo kunaonekana kwa haraka ili uweze kuifanya ngozi yako iwe na mvuto wa kupendeza.
Liwa haichubui uso wala kukufanya uwe mweupe, bali liwa inakufanya ngozi yako ing’are zaidi na kukuweka katika hali ya kupendeza wakati wote.

Unashauriwa kuwa na utaratibu wa kuacha ngozi yako ipumzike wakati wa usiku bila kuweka kitu chochote chenye kemikali kwa ajili ya kufanya ngozi yako iwe nyororo na ya kupendeza maana mchana huwa inasinyaa kutokana na joto la jua.

Ukitaka kumwandaa bibi harusi, liwa hupakwa kabla ya wiki nzima kwa ajili ya kumwandaa kwa sherehe ya kwenda kuolewa yaani njia ya kumwandaa bibi harusi kabla ya kuolewa.

Liwa hupakwa bila ya kujali kuwa wewe ni mweupe au ni mweusi yaani haichagui mtu wa kutumia kwa kuwa ni kwa ajili ya kung’arisha tu na wala si kwa ajili ya kujichubua. Liwa inaweza kupakwa kutwa mara mbili au hata zaidi kwa kuwa haina madhara yoyote katika ngozi ya binadamu ila inakufanya uwe mwororo na mwenye kuvutia zaidi.

Liwa ikichanganywa na ‘tumeric’ na viazi hufaa kupaka wanawake na wanaume wanaopenda ngozi zao kung’aa na kupendeza.








KUATHIRIKA KISAIKOLOJIA
Na John Chikomo-Mratibu wa Afya ya Akili Manispaa ya Kinondoni
Yaliyomo
1.     Utangulizi
2.     Nini maana ya kuathirika kisaikolojia
3.     Aina za athari za kisaikolojia
4.     Athari za kawaida za kisaikolojia
5.     Athari zisizo za kawaida za kisaikolojia
6.     Matokeo ya athari za kisaikolojia kwa familia na marafiki
7.     Matokeo ya athari za kisaikolojia kwa jamii
8.     Matokeo ya athari za kisaikolojia kwa watoto

1.     UTANGULIZI
Watu wengi wamekuwa wakitumia neno Matatizo ya kisaikolojia katika maisha ya kila siku wakimaanisha hali ya mtu mwenye tabia na mwenendo tofauti katika jamii. Lakini ufunguo wa kujua matukio ya matatizo ya kisaikolojia  ni hali ya mtu kuwa na msongo mkubwa wa mawazo ambayo mtu anashindwa kukabiliana nayo. Wataalam mbalimbali katika taaluma wanaelezea matatizo ya kisaikolojia katika mitazamo mbalimbali.
Ninachojaribu kukikazia katika somo hili ni kwamba mtu binafsi ndiye anayeweza kuelezea vizuri kuwa tukio lililompata limemuumiza au lah.
2.     Hivyo tafsiri ya kuathirika kisaikolojia ina mapana yake, inajumuisha miitikio yenye nguvu ya matukio mengi ya kuumiza kama; ajali, majanga asilia, ukatili, kufanyiwa upasuaji, umaskini, kuachika/kuachana, magonjwa, kukataliwa na mzazi, kubakwa, uharifu wa kutumia silaha, mafuriko, kukosa ajira, kufiwa na mpenzi, ulemavu na, kutukanwa.
Moja kati ya watu niliowahi kuzungumza nae, akiwa katika kujieleza yanayomsibu alisema “Baada ya jambo hili kunitokea nilijihisi kama nimetwishwa mzigo mkubwa sana kichwani kwangu, muda wote”
Pamoja na kwamba matukio yote hayo yaliyotajwa hapo juu yanaumiza, lakini lakini siyo yote huitwa kuathirika kisaikolojia. Lakini mengine huitwa mapitio ya kisaikolojia (Traumatic experiences), na mapitio haya ya kisaikolojia huwa inakuwa ya ghafla na ya-kushtua, na inahusisha hatari na hisia ya woga, na kukosa matumaini.
Kwa Mfano, mama mmoja tukiwa katika mazungumzo, mbali na mambo mengi aliyoelezea akijaribu kuonyesha hatua aliyofikia alisema “nilidhani huo ndio ulikuwa mwisho wa maisha yangu, nisingewaona tena wanangu”.
Tofauti kati ya kuathirika kisaikolojia na kupata tukio la ghafla lenye maumivu ndiyo inayotoa dira ya namna ya kumsaidia mtu wakati wa kumpatia msaada wa kitaalam.
3.     AINA ZA ATHARI ZA KISAIKOLOJIA
a)    Single traumatic experience;- katika aina hii, mtu anakuwa amekutana na tukio moja kwa mara ya kwanza. Mfano ameshuhudia mtu akiuawa.
b)    Multiple trauma;- Mtu anakuwa amekutana na matukio mengi ya kuumiza. Mfano mtu amepata ajali za gari mara kadhaa na kuvamiwa na watu wenye siraha.
c)     Continuous trauma;- katika aina hii mtu anakuwa anaishi katika eneo ambalo kuna matukio ya kutisha na yanaendelea katika eneo hilo. Mfano nchi yenye mchafuko wa kisiasa wananchi wanaishi mazingira ya hatari kwa miaka mingi wakishuhudia matendo ya kikatili. Au askari ambae anafanya kazi katika mazingira hatarishi ya vita kwa muda mrefu.
d)    Complex trauma;- hii hutokea katikati ya watu wenye mahusiano maalum, kwa mfano ukatili wa kijinsia baina ya wana-ndoa, ndugu n.k.

4.     ATHARI ZA KAWAIDA ZA KISAIKOLOJIA

Baada ya mtu kuishi katika hali ya mawazo na maumivu yasiyopata utatuzi kwa muda mrefu, ndipo athari za kisaikolojia huanza kujitokeza “kuathirika kisaikolojia kunakufanya uvunjike moyo kwa ndani-kama nguo iliyochakaa’’. Zifuatazo ni baadhi za athari za kawaida za kisaukolojia;

                        i.         Mawazo ya kila wakati kuhusiana na tukio
                      ii.         Kuona, kusikia, au kuhisi harufu ambayo inafanana na tukio
                    iii.         Ndoto za usiku
                     iv.         Kukosa usingizi
                       v.         Kuanza kutumia dawa za kulevya
                     vi.         Kuongea kuhusu tukio lililokupata kila wakati
                   vii.         Mwili kuuma
                 viii.         Huzuni na kulialia
                     ix.         Kutaka kulipiza kisasi
                       x.         Hasira na sonona
                     xi.         Kuviepuka vitu vinavyoshabihiana na tukio
                   xii.         Kujiona hana thamani
                 xiii.         Kujitenga
                   xiv.         Kutomwamini yeyote.

Itaonekana ni ajabu, sio ya kawaida, ya kushanagaza na kushtua sana kuona mtu kama anakutana na tukio la kutisha halafu asionyeshe mwitikio wowote kati ya hizi zilizotajwa hapo juu.
Athari ikizidi kuwa kubwa zaidi  na ya kutisha na yenye maumivu, mtu kwa kawaida hujaribu kuonyesha mwitikio kati ya aina hizi mbili zifuatazo;
a)    Kuepuka;- mtu anajitahidi asikumbuke tukio lililompata, mahali pa tukio na kuepuka kitu chochote kinachoshabihiana na tukio. Mtu anajilinda kutokuongelea tukio na kuanza kutumia vileo au dawa ili kuzuia mawazo yanayomsumbua, na wakati mwingine tatizo likidumu kwa muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi anapoteza uwezo wa kusikia na kuongea.

b)    Kujirudia;- Mara nyingi matukio ya kutisha huwa na tabia ya kujirudiarudia kwenye ufahamu wa mtu. Hii hutokea kwa njia ya kuwaza na kuota ndoto zinazohusiana na tukio. Jambo hujirudia kwenye akili ya mtu lakini mlengwa hataki, hivyo hujikuta anaingia kwenye mgongano wa mawazo  (hataki kuwaza lakini yanakuja). (approach avoidance conflict).


5.     ATHARI ZISIZO ZA KAWAIDA ZA KISIKOLOJIA
a.    Hallucinations (mareweruwe): kusikia, kuona au kuhisi vitu ambavyo kiuhalisia havipo.
b.    Delusions (dhana potofu): anang’ang’ania vitu ambavyo havina ukweli na kuvisimamia kwa gharama yoyote na wala huwezi kumuhamisha katika mawazo hayo.
c.     Severe depression: sonona iliyozidi
d.     Kuwa mchangamfu kupita kiasi, kuwa na matumizi makubwa ya fedha, kuwa na furaha kupita kiasi.
e.     Kuwa na matukio ya kutaka kujiua.

6.     MATOKEO YA ATHARI ZA KISAIKOLOJIA KWA FAMILIA NA MARAFIKI
-Matokeo ya athari hizi huwa zinaenda mbali zaidi ya mtu mwenyewe, kama kitu kibaya cha kuumiza kikitokea ndugu jamaa na marafiki pia huathirika. Hii ilithibitishwa na mama mmoja ambaye binti yake alibakwa, alionyesha hisia zake kwa kusema “Najua nimekuwa muoga sana juu ya binti yangu, hasa ninapokumbuka kuwa binti yangu amebakwa, nadhani mi naumia na nawaza zaidi kuliko yeye na matumaini yangu yote juu yake yamefifia”.

Mfano mwingine: mwanamke mmoja alikuwa akitoa maelezo juu ya hali iliyompata mume wake; “tangu amevamiwa na majambazi amebadilika sana, anakaa tu na hataki hata kuongea na mtu. Na wakati mwingine hutufokea bila sababu maalum, watoto wameshajifunza kukaa nae mbali kwa hofu”.

Mara nyingi watu walioumizwa kisaikolojia hujisikia vibaya wanapohisi kama familia au marafiki hawajalipokea vizuri jambo lake, hivyo huwafanya kuwa makini sana na watu wengine, na wakati mwingine huamua kuwaficha hata watu wa karibu sana juu ya mambo yanayowatokea kwa kuhofia wasije wakailetea huzuni familia.
Familia na marafiki hujisikia vibaya, wenye hasira na lawama nyingi juu ya aliyefanya ukatili dhidi ya ndugu yao.

7.     MATOKEO YA ATHARI ZA KISAIKOLOJIA KWA JAMII
-uwezekano wa mtu akipatwa na jambo baya, jamii nayo kuathirika na hali hiyo ni mkubwa.  Na jamii yetu mara nyingi inashindwa kutoa msaada kwa watu waliopatwa na matatizo kama ya kubakwa na aina nyingine nyingi za ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.
Yafuatayo ni maelezo ya mtu aliyetendewa jambo la kikatili la kubakwa, na jamii badala ya kumtia moyo imekuwa ikimsema vibaya na kumtenga. Kwa maneno yake alisema: kitu kinachonisikitisha na kuniumiza moyo wangu ni namna jirani zangu, wanaofahamu yaliyonipata wanavyonitazama, Nimekuwa nikiwaona wananiteta na wamekuwa wakiniepuka”.
-matokeo ya kuumizwa kisaikolojia kwa jamii ya karibu, kama vile shule, makanisa na misikitini, lisichukuliwe kwa wepesi; watoto waelimishwe, na wazazi pia lazima wapate muda wa kuzungumzia mambo yahusuyo matukio magumu yaliyowapata kifamilia.
-wakati mwingine jamii yote huathirika na majanga ya asili kama vile; mafuriko, au vurugu za kisiasa ambazo hudumu kwa muda mrefu. Makundi haya pia yanahitaji unasihi wa karibu.

8.     MATOKEO YA ATHARI ZA KISAIKOLOJIA KWA WATOTO
·       kwa watoto wadogo huanza kunyonya vidole au kuongea kama katoto kachanga
·       wanakuwa na hasira na kujitupatupa chini au kugalagala.
·       Watoto wengi hujaribu kutaka kupata msaada kwa kujisingizia kuumwa; kichwa, tumbo, au mguu ili mradi asikilizwe.
·       Huepuka kwenda maeneo ambapo tukio lilimpata, na pia huepuka hata chakula ambacho alikula siku ya tukio au hukataa kuvaa nguo aliyovaa siku ya tukio.

Kuathirika kisaikolojia sio jambo la kujitakia, linaweza kumpata binadamu yeyote anayeishi katika dunia hii iliyojaa mambo mengi. Hivyo mara tu upatapo jambo gumu linalokosa majibu au utatuzi wa haraka, usisubiri mpaka ukose usingizi, ushindwe kula na watu kukuona umeshaanza kuwa sio wa kawaida. Tafuta msaada, kwani MAWAZI YAKO SIO MWISHO, TAFUTA MSAADA.

UMUHIMU WA TENDE KWA AFYA YAKO
Na Seif Oddo
IMEZOELEKA kuwa tende hutumika katika kipindi cha mwezi wa Ramadhani na waumini wa dini ya Kiislamu. Tunda hili limethibitishwa kuwa na manufaa makubwa katika mwili wa binadamu likitumiwa vizuri.

Tunda hilo ni maarufu sana katika nchi za Mashariki ya Kati na sehemu nyinginezo duniani.

Asili ya tunda hili ni nchi za Kiarabu, na liliingia Afrika Mashariki katika karne ya 7. Hapa nchini, tende hupatikata kwa wingi visiwani Zanzibar na Pemba, ambapo imekuwa kama ni sehemu ya chakula cha kiutamaduni visiwani humo.

Mbali na ladha yake kuwa nzuri na yenye kuvutia, yenye kufanya watu wengi kulipenda tunda hili, tende pia limekuwa likitajwa sana katika vitabu vitukufu vya dini.
Waumini wa dini ya Kiislamu wamekuwa wakitumia tende kwa wingi, sana hasa katika kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Shekhe Khalfan Tiwanywa wa Chakechake, Pemba anaeleza kuwa, “tende ni moja ya vyakula vilivyotajwa katika Quraan Tukufu.”

Anaongeza kwa kusema kuwa, katika kisa maarufu cha kuzaliwa Nabii Issa, mama yake Nabii Issa (Bi. Maryam) aliamriwa kula tende baada ya kujifungua, ili kurudisha damu nyingi aliyoipoteza baada ya kujifungua pamoja na kurudisha nguvu ya mwili wake kwa haraka.

Mbali ya kuwa na ladha ya kuvutia, tende ina manufaa mengi mazuri kiafya katika miili yetu.

Wataalam wa tiba wamethibitisha kuwa tende ni chanzo cha virutubisho na nishati mwilini. Pia huwezesha mwili kupata nguvu kwa haraka.

Hii inaendana na sababu ya tunda hili kutumika kwa wingi katika Mfungo wa Ramadhani, kwani waumini waliofunga hulitumia tunda hili kurudisha nguvu na nishati iliyopotea mchana kutwa walipokuwa wamefunga.

Wataalam wanaendelea kueleza kuwa, ndani ya tende kuna virutubisho kama vile calcium, protein, potassium, magnessium, phosphorous, vitamin A, folate na cabohydrates ambazo zote kwa pamoja ni muhimu katika miili yetu kiafya.

Dk. Ally Khamis wa Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja kisiwani Zanzibar ameeleza kuwa, tende ni chakula cha afya na ina mkusanyiko wa vitamin A ambayo husaidia katika kuongeza nuru ya macho. Pia kuna madini ya kalishi ambayo husaidia kuimarisha mifupa. Vilevile, kuna vitamin B6 na B12 ambazo husaidia katika usagaji na ufyonzaji mzuri wa chakula na kuingia katika mishipa ya damu.

Wataalam wamegundua kuwa tende hutoa kinga dhidi ya maradhi ya saratani ya tumbo (colon cancer). Pia ina uwezo wa kuimarisha moyo na kuukinga dhidi ya maradhi.

Mbali na hayo, tende pia hutibu maradhi ya tumbo kama vile kujaa gesi, kuharisha na kuchafuka kwa tumbo. Pia wataalam wanaeleza kuwa tende husaidia kuondoa sumu mwilini na kusaidia kuongeza nguvu za kiume ikitumiwa kwa kufuata ushauri wa kitabibu.

Tende ni tunda pekee lenye uwezo wa kuupa mwili vitu vinne kwa wakati mmoja ambavyo ni protini, wanga, vitamin na mafuta.

Pia tende ni tunda ambalo huyeyuka haraka sana tumboni, hivyo kutolipa tumbo shida ya kufanya umeng’enyaji (digestion).

Wataalam wa afya wameeleza kuwa, tunda hili husaidia kutanua misuli ya mji wa mimba na hivyo basi humsaidia mwanamke kutopoteza damu nyingi wakati wa kujifungua. Wataalamu hawa wanaendelea kueleza kuwa, tende ni chakula bora kwa wanawake wanaonyonyesha kutokana na kusaidia kuyapa maziwa virutubisho muhimu ambavyo humfanya mtoto kuwa na afya bora.

Kutokana na uwepo wa madini chuma ndani ya tende, husaidia kuwapa ahueni watu wenye upungufu wa damu mwilini.

Hivyo basi, mbali na kupenda kuitumia tende kipindi cha Mwezi wa Ramadhani tu, ni vema tukaitumia siku zote kama jinsi tunavyotumia vyakula vingine, ili kuweza kuimarisha afya zetu kikamilifu.


KUTOKA KIUMBE TRADITION AND MEDCINE RESEARCH
MAAMBUKIZI YA KATIKA NJIA YA MKOJO (UTI)
Na Dk. Karama Kiumbe
Karibu mpenzi msomaji wa TABIBU katika safu hii kutoka Kiumbe Tradition and Medcine Research. Leo tutazungumzia tatizo la maambukizi ya katika njia ya mkojo kwa jina la kitaalam huitwa ‘Urinary Tract Infection (UTI)’.
Leo tutaangazia mambo yafuatayo katika tatizo hili linalowasumbua Watazania wengi;-
1.    Maana ya U.T.I
2.    Sababu za U.T.I
3.    Dalili za U.T.I
Maana ya U.T.I
Maambukizi katika sehemu yeyote ya njia ya mkojo husababisha maradhi na matatizo ya aina mbalimbali. Mara nyingi tunapozungumzia UTI, huwa tunalenga maambukizi yanayosababishwa na vimelea (bacteria) au chochote kile kinachoweza kusababisha 

UTI kinapoingia katika njia ya mkojo kutokea aidha nje ya mwili au hata ndani ya mwili kwa njia ya damu au vinginevyo.

UTI huweza kumpata mtu yeyote bila kujali jinsia au umri. Hata hivyo, yapo makundi ambayo kutokana na sababu za kibayolojia na kinga ya mwili kushuka au kuwa ndogo, huathiriwa zaidi na tatizo hilo. Makundi hayo ni pamoja na watoto, wazee na wanawake.

Watoto ni waathirika wakubwa wa UTI na yaweza kusababisha maambukizi kusambaa hadi kwenye damu na mwili mzima na hatimaye kusababisha kifo. Maumbile ya watoto na utegemezi walio nao wakati wa kujisaidia inaweza kuwa ni sababu hatarishi kwa wao kupata tatizo hili. Vile vile kinga yao ya mwili bado huwa haijakomaa kuweza kuhimili uvamizi wa vijidudu mbalimbali kwenye miili yao.

Wanawake kwa upande wao huathiriwa na UTI hasa kutokana na mfumo mzima wa maungo yao hasa ya mfumo wa mkojo kuwa na urahisi wa kuingiliwa na bakteria. Mathalani, mrija wa mkojo yaani ‘urethra’ ya mwanamke ni fupi sana ukiliganisha na ya mwanaume na hivyo vijidudu au bakteria kupata urahisi wa kuingia ndani.

Sababu za UTI
Kuna sababu nyingi zinazoweza kupelekea mtu kupata tatizo hili; kutokana na mazingira na maumbile, umri, jinsia na mfumo wa kibaolojia. Miongoni mwa sababu hizo ni kutokunywa maji mengi kwani binadamu kwa siku anahitajika kunywa angalau lita tano za maji, matumizi ya maji machafu wakati wa kujisafisha au kuoga, kuvaa nguo chafu hususan nguo za ndani pamoja na kufanya ngono isiyo salama.

Dalili za UTI
Dalili zinaweza kuwa kusikia maumivu wakati wa kukojoa, homa na maumivu katika viungo vya mkojo, kuhisi kuhitaji kukojoa mara kwa mara na pia mkojo kuwa na hali ya kuunguza wakati wa kukojoa.

Nyingine ni maumivu ya tumbo chini ya kitovu au mgongo kwa chini. Mkojo wenyewe unaweza onekana wenye damu au usaha. Wakati mwingine, mtu anaweza kupatwa na shinikizo la chini la damu.

Mpenzi msomaji usikose toleo lijalo kwani tutaanza kuzungumzia tatizo hili kulingana na makundi, yaani U.T.I kwa watoto, wanawake, wanaume na kwa mama wajawazito kwa mapana zaidi.
Kwa mawasiliano na huduma nyingine za kiafya na ushauri, fika ofisini kwetu iliyopo Ukonga Mongo la Ndege - Njiapanda ya Segerea, Dar es Salaam au tupigie kupitia 0715 112 131.
            



MARADHI YATOKANAYO NA NYAMA ZA WANYAMA
Na Dk. Geoffrey C. Lusanzu

Kwa walio wengi, ulaji wa nyama ni jambo lisiloshtua mioyo kutokana na mazoea ya ulaji wa chakula hiki.

Wengi wetu chakula cha nyama ni kitamu sana na inaweza kushangaza mno endapo utaandaa sherehe isiyokuwa na mlo wa nyama, lakini kiutaalam nyama sio chakula rafiki wa mwili wa mtu kwa kuwa ina tindikali. Mwili ni alikalaini, kwa maana hii nyama ni mpinzani wa mwili.

Licha ya kutokuwepo upatanifu huu, nyama za wanyama na samaki zina kiwango kikubwa cha lehemu ambayo ni mafuta mabaya (cholesterol). Mafuta haya yanapouzinga mwili, huharibu damu, misuli ya damu na viungo vya mwili na husababisha maradhi makali na kifo.

Jamii ya wanyama inaugua mno na hata wanapochinjwa nyama zao hukokota vimelea vya maradhi lukuki.

Kwa kawaida, nyama inapoliwa huingia tumboni na huoza huku ikitengeneza usaha unaonuka (putrid mass), kisha hufyonzwa na kuingia katika mkondo wa damu na kuidhoofisha damu.

Daima ni tabia ya nyama kuidhoofisha damu kwa kiwango kikubwa.

Tafiti mbalimbali zimethibitisha vema kwamba ulaji wa nyama za aina zote (wanyama, samaki na ndege) ni hatari kwa afya ya binadamu kwa sababu nyama zimesheheni vimelea wengi wa maradhi.

Ni wanyama kama ndege na samaki wachache ambao hawajaambukizwa maradhi. Kutokana na tafiti hizi binadamu anaweza kuendelea kula nyama za wanyama kwa hasara ya nafsi yake kwani vimelea wa maradhi hawana utani au urafiki na mtu yeyote.

Hii ni kwa sababu huweza kuharibu afya ya mtu yeyote pasipo kujali rika, elimu, madaraka, utajiri au umasikini.

Je, ni maradhi gani yanayopatikana kwa ulaji wa nyama?
Haijalishi unakula nyama kwa kiwango kipi; kidogo au sana kabisa. Hata ulaji wa nyama wa kawaida unaweza kukusababishia ugojwa mkali na kupelekea ulemavu au kifo cha mapema.

Nyama ina wadudu wabaya kama vile bakteria, ‘salmonella’, ‘listeria’, ‘campylobacter’, ‘clostridium’, ‘perfringens’ na ‘yersinia. Vimela hawa huweza kusababisha maradhi ya minyoo ndoano (hookworms), ‘rabies’, kipindupindu, tegu ya samaki, tegu ya nguruwe, kuhara damu, maradhi makali ya figo, baridi yabisi na maradhi ya ini.

Maradhi mengine yanayotokana na ulaji wa nyama ni gauti, vijiwe katika kibofu nyongo na figo, kichwa kuuma na kisichosikia dawa, saratani ya damu (leukemia). Pia husababisha saratani nyingine zaidi ya kumi (melanoma na ‘lymphoma’), ukichaa (mad cow disease).

 Saratani ya tezi dume (prostate cancer), saratani ya tumbo, mfumo wa kinga ya mwili dhaifu, kirusi cha hunta, maradhi ya Hodgkin, maradhi ya ‘paget’, ‘leptospirosis’, homa kali pamoja na kuvimba (bubonic plague), ‘anthrax’, ‘trichinosis’, minyoo mviringo (round worms), ‘brucelosis’, kifua kikuu, ukoma.

Magonjwa mengine ni kifafa, homa kali, matutuo, akili butu, tegu wa ng’ombe, minyoo midogo iliyobapa (ring worms), hali ya unyama na uzezeta, homa kali pamoja na uvimbe (tularemia), kuharisha maji na kuumia tumbo (cryptosporidiosis).

Maradhi yote haya humwinda binadamu mlaji wa kitoweo cha nyama.

Wakati umefika sasa wa kutafakari, kupunguza ulaji wa nyama au kuanza kusaka elimu ya afya ili kujikita katika matumizi ya chakula mbadala wa nyama na kukiacha kabisa chakula cha nyama.

Daima tumia chakula bora cha asili ili kujikinga na maradhi haya yaliyo hatari mno na yanaleta vifo vya mapema mno.     



TATIZO LA UPUNGUFU WA MBEGU ZA KIUME
(OLIGOSPERMIA)
 KUTOKA VICTORIA THERAPIES

Oligospermia ni ile hali ya manii ambayo mwanaume huyatoa baada ya kufika kileleni kubeba mbegu chache ambazo ziko chini ya million 15 katika kila mililita ya manii.

Uzalishaji wa mbegu za kiume ni mchakato unaohitaji korodani ambazo zina afya nzuri na zinafanya kazi vizuri, pamoja na ‘hypothalamus’ ambayo ni sehemu ya ubongo na ‘pituitary grand’, tezi ilyopo kwenye ubongo inayozalisha vichocheo vinavyosaidia uzalishaji wa mbegu za kiume.

Endapo mbegu za kiume zitazalishwa na korodani, zinasafirishwa na mirija (vas deference) na kuchanganyikana na manii na kuwa pamoja. Mchanganyiko huo unatoka nje wakati wa kujichua au tendo la ndoa.

Kwa sababu mbalimbali zinazoweza kusababisha mbegu za kiume zisiwe na umbo linalotakiwa, speed, afya nzuri na wingi unaotakiwa kiasi kwamba zinaweza kushindwa kurutubisha yai la mwanamke.

1.    Maambukizi katika korodani yanayotokana na vimelea mbalimbali (bacteria) vinavyoweza kushambulia korodani na kuzifanya zishindwe kuzalisha mbegu zenye afya nzuri.
2.    Retrograde ejaculaition: ni ile hali ya mbegu za kiume na manii kuingia katika kibofu cha mkojo wakati wa kufika kileleni baada ya kutoka nje au kuingia kwenye uke. Chanzo cha tatizo hili ni sukari ya kupanda. Mtu ambaye ana tatizo kwenye uti wa mgongo hufanyiwa upasuaji wa tezi dume na kibofu cha mkojo na inaweza kupelekea mbegu kuingia katika kibofu cha mkojo badala kutoka nje.
3.    Chanzo kingine ni zile seli za kinga za mwili kuzitambua mbegu za kiume kama ni adui katika mwili na kuzishambulia na kuzifanya zikose ubora wa kuweza kurutubisha yai.
4.    Kutoshuka kwa korodani (undescended testicles) ni tatizo lingine linaloweza likaathiri utendaji kazi wa korodani kwa sababu ya joto la mwili kuwa kali kuliko joto ambalo linatakiwa liwe katika korodani, hatimaye kupelekea korodani kushindwa kuzalisha mbegu zilizo bora.
5.    Matatizo ya vichocheo (hormone) ‘hypoltupituitary’ na korodani huzalisha homoni ambazo ni muhimu kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu za kiume. Mfano ‘testosterone hormone’ isipotolewa, mbegu zitakazotolewa zitakuwa kidogo na zisizo na ubora.
6.    Mazingira yanayopelekea korodani ziwe na joto kali kama kukaa kwa muda mrefu, kuvaa nguo za kubana, kutumia laptop ikiwa mapajani kwa muda mrefu inaweza pia kuongeza joto kwenye korodani na kupunguza uzalishaji wa mbegu za kiume.
Pia kuendesha baiskeli kwa muda mrefu ni chanzo kingine kinachosababisha kuongezeka kwa joto katika korodani na kufanya ushindwe kuimarisha mbegu kwa wingi na ubora.
7. Utumiaji wa madawa ya kulevya kama vile ‘cocaine’, bangi, ‘steroid’ ambazo husababisha korodani kushindwa kuzalisha mbegu bora.
8. Ulevi wa pombe na uvutaji wa sigara unaathiri uzalishaji wa ‘testosterone hormone’ inayosaidia uzalishaji wa mbegu za kiume.
9. Msongo wa mawazo pia unaweza ukaathiri uzalishaji wa homoni zinazosaidia uzalishaji wa mbegu za kiume
10. Unene uliopitiliza ni chanzo kingine kinachopelekea homoni zisitolewe kwa wingi hatimaye kusababisha uzalishaji wa mbegu za kiume kuzorota.

Dalili za tatizo
·      Kushindwa kurutubisha yai la mwanamke ambalo lina afya.
·      Uume kusimama legelege
·      Maumivu na kuvimba kwa korodani
·       Manii kutoka kidogo sana na mepesi wakati wa kufika kileleni.

Matibabu ya tatizo
Yanategemea korodani au viungo vingine vinavyosaidia uzalishaji wa mbegu za kiume, vimeathirika kiasi gani na chanzo cha tatizo ni nini. Kwa hiyo, mwanaume yeyote ambaye umeishi na mwanamke zaidi ya mwaka mmoja bila kusababisha ujauzito na una dalili zilizotajwa hapo juu nenda hospitali kupima au tutembelee 

Victoria Therapies iliyoko Mtoni Kijichi, Temeke, jijini Dar es Salaam. Pia unaweza wasiliana nasi kupitia 0658 027 027 kwa ajili ya vipimo, matibabu na ushauri.



UGONJWA WA TUNDU KATIKA MOYO KWA WATOTO – 2

Na Dk. Fadhily Emily
Karibu msomaji wa gazeti TABIBU. Wiki iliyopita tulizungumzia jinsi ugonjwa wa tundu katika moyo wa mtoto unavyoweza kutokea, pamoja na dalili zake. Leo hii, tuangalie madhara ya ugonjwa huu na tiba tofauti zinazotumika kumaliza tatizo hili.
Madhara ya Tundu Katika Moyo
Madhara ambayo yanaweza kusababishwa na tundu katika kuta za chini za moyo ni Eisenmenger Syndrome, hali ambayo hutokea pia pale mtu anapokuwa na tundu katika kuta za juu za moyo.
Tatizo hili hutokea wakati mtiririko wa damu unaongezeka kutoka kushoto kwenda kulia kupitia tundu katika kuta za moyo, suala ambalo huongeza mtiririko wa damu katika mishipa ya mapafu na kusababisha shinikizo la damu katika mapafu. 


Hali hii husababisha ongezeko la shinikizo la damu katika upande wa kulia wa moyo na kubadilika kwa shanti kutoka kulia kwenda kushoto. 



Matokeo yake ni kuwa damu isiyo na oksijeni iliyotakiwa kwenda kwenye mapafu kwa ajili ya kusafishwa, huchanganyika na damu yenye oksijeni iliyoko upande wa kushoto na kusambaa mwilini. 

Madhara mengine ya tundu la VSD ni kupata ugonjwa wa kiharusi, moyo kushindwa kufanya kazi vizuri, pia maambukizi katika kuta za ndani za moyo (endocarditis), ugonjwa ambao tutauelezea katika matoleo yajayo. 



Akina mama waliozaliwa na tatizo hili, ambao wametibiwa na hawakupata madhara wanaweza kushika mimba na kupitisha kipindi cha ujauzito bila matatizo yoyote. 

Wale ambao hawakutibiwa au ambao tayari wameshapata madhara, hushauriwa kutoshika ujauzito kwa sababu ya hatari zinazoweza kutokea katika kipindi cha ujauzito.

Vilevile, kwa akina mama waliozaliwa na tatizo hili, uwezekano wa watoto wao kuzaliwa na tatizo hili huwa mkubwa. 



TIBA

Inafaa kujua kuwa, karibu nusu ya wagonjwa wenye tatizo hili huwa hawahitaji matibabu ya aina yoyote ile kwa kuwa tatizo hili hujirekebisha katika miaka ya mwanzo ya maisha yao. 

Hata hivyo, kwa wale ambao watahitaji matibabu, hutibiwa kwa dawa au upasuaji kwa kutegemea ukubwa wa tatizo lenyewe. 



Dawa zinazotumika kutibu ugonjwa huu ni zile ambazo hupunguza kasi ya moyo, huongeza nguvu ya mapigo ya moyo na zile ambazo hupunguza maji mwilini au ‘diuretics’. 

Utaratibu wa kuziba tundu umegawanyika katika sehemu mbili na hufanyika iwapo tundu ni kubwa sana, au halikujirekebisha lenyewe wakati mtoto alipokuwa anakua na pale ikiwa dawa alizopewa mgonjwa hazikusaidia. 



Pale inapohitajika upasuaji, mgonjwa hufanyiwa oparesheni ambapo kifua hufunguliwa ili kuziba tundu la VSD. 



Matibabu mengine ni kupitisha mrija katika mshipa wa damu hadi katika sehemu ya tatizo kwenye moyo na kuliziba kwa kutumia kifaa maalum. Kwa njia hii, huwa hakuna haja ya kufanya upasuaji wa kufungua kifua cha mgonjwa.



FAHAMU MUZIKI TIBA
Na Kennedy Chaya
IMEELEZWA kuwa muziki ni tiba ya Magonjwa mbalimbali yanayomsumbua mwanadamu katika maisha yake ya kila siku.

Swali la kujiuliza ni kwamba ni aina gani ya muziki unauzungumziwa hapo  kuwa ni tiba kwa  mgonjwa.

Muziki tiba(Polyphonic  Muzic Therapy) huu ni aina ya muziki  maalum ambao unatumika  kama tiba ya magonjwa.

Magonjwa kama  ya Presha msongo wa mawazo,vidonda vya tumbo,Sukari na magonjwa mengine mengi.

Muziki huo  pia ukitumika vizuri unaweza kuwaondelea uchovi watu mbalimbali husani wafanyakazi maofisini baada ya kazi ya kutwa nzima sambamba na wanafunzi baada ya kumaliza vipin di  vyao vya darasani.

Muziki  tiba uligunduliwa katika  karne ya 20 huko Marekani ambapo  kwa sasa  tiba hiyo katika mataifa yaliyoendelea wanaitumiakwa ajiri ya kujenga afya zao.
Dk.Susan Hadley   Mhadhili wa kozi ya Muziki  tiba  kutoka chuo cha Rock 

University kilichopo nchini  Marekani aliwahi kusema kuwa mtu hawezi kutubiwa na kupona magonjwa yake kwa dawa pekee hata pia kwa tiba ya Muziki mtu anaweza kupona ugonjwa wake.

Aliongeza kuwa  magonjwa mengi yanayowapata bianadamu wengi yanatibika kwa muziki hivyo tiba ya muziki ni muhimu kwa wagonjwa.

Aidha Dkt Suzan kama Mtaalum wa muziki tiba alifafanua kuwa ni muhimu pia kufikiria mahali pa kuweka kituo au hospitali ya tiba hiyo kwani inahitaji eneo tulivu kusiwe na mwingiliano na kazi za kijamii au sehemu zenye kelele nyingi.

Katika nchi za Uingereza,Marekani tiba hiyo ni maarufu sana zipo hospital maalum na vituo kwa ajiri ya tiba  hiyo ambapo watu huenda kupatiwa huduma hiyo  ya kupigiwa muziki huo mpaka mgonjwa anapona.

Ileweke wazi kazi ya muziki huo ni kuburudisha nafsi kama inavyoeleweka kuwa nafsi inabeba mambo mengi hivyo ikitiburiwa huleta magonjwa mbalimbali hivyo tiba yake halisi ni Poly phonic(muziki tiba).

Wakati  umefika sasa kwa nchi zinazoendelea  kama Tanzania kuwa na vituo au hospitali  kwa ajiri ya kutoa tiba hiyo ya muziki ili kufanya maisha yao yaendelee kuwa na uhakika.






FAIDA ZA KULA TANGO NA TIKITI MAJI
Na  Zamda Haroun.

Tikiti maji  na matango ni aina ya matunda ambayo hupatikana kwa wingi hapa nchini,

Kwa karibu mikoa mingi ya Tanzania bara zao hili hulimwa kama zao la chakula lakini pia kama zao la biashara,mazaoa hayo yana faida nyingi katika mwili wa binadamu kama inavyoelezwa na watalaamu wa afya

Faida mojawapo ya Ulaji wa matango  na matikiti maji husaidia kuboresha kiwango cha maji ambayo huitajika mwilini, hii ni kutokana na matango kuwa na kiwango kikubwa cha maji ambayo husaidia kuondoa taka mwilini.

Sambamba na hilo matango na tikiti maji huondoa  sumu mbalimbali ambazo miili yetu huzipata kupitia vyakula, madawa na hata vinywaji.

Husaidia pia kupunguza uzito wa mwili. Kutokana na kuwa na    asili ya nyuzi nyuzi au, fibres, humfanya mlaji ajisikie kushiba bila ya kuongeza vitu mwilini ambavyo husababisha mtu aongezeke uzito hivyo kuzuia magonjwa mbalimbali.

Lakini pia hupunguza (hangovers),uchovu  pamoja na hali ya kujisikia vibaya kutokana na unywaji wa kilevi. Hii ni kutokana na kuwa na vitamini B na maji mengi ambapo, baada ya mtu kunywa kilevi na kisha akaja kula matango kabla ya kulala, itamfanya asubuhi asiamke huku akiwa na hangovers.

Faida nyingine husaidia katika mmeng’enyo wa chakula, matatizo ya tumbo kama vile kuvimbiwa, tumbo kujaa gesi, vidonda vya tumbo na mengineyo hupungua kutokana na ulaji wa matango,

Ulaji wa matunda hayo husaidia kuondoa sumu tumboni na kurahisisha ufyonzwaji wa protein mwilini kutokana na uwepo wa kiwezeshaji cha kibaiolojia kinachoitwa, erepsin enzyme.

Aidha Matango na Matikiti maji husaidia kuondoa msongo wa mawazo kwani yana kiwango kikubwa cha vitamini B ambayo husaidia  utendaji kazi wa mishipa mbalimbali ya fahamu mwilini na hivyo kuondoa hatari ya mtu kuathirika na msongo wa mawazo unaosababishwa na maisha ya kila siku.

Matunda hayo huondoa pia hatari ya mtu kupata kansa, kwani yana kiwango kikubwa cha virutubisho vyenye asili ya mimea viitwavyo, lignans, ambavyo pamoja na vitamini c, husaidia kuondoa sumu mbalimbali na kuiboresha kinga ya mwili na hivyo kuepusha hatari ya mtu kupata kansa. 

Sambamba na hilo husaidia kuondoa harufu mbaya kinywani Kwa kukiweka kipande cha tango mdomoni kwa dakika kadhaa, huuwa bakteria mbalimbali wasababishao magonjwa mbalimbali ya kinywa na harufu mbaya mdomoni. 

Husaidia mtu kupata choo laini na huzuia kukosa choo. Huzuia pia kuganda kwa mafuta katika mishipa ya damu ili kuwezesha mzunguko sahihi wa damu kaitikpande zote za mwili sambamba na kurekebisha mapigo ya moyo.
Huwepo wa vitamini katika matunda haya husaidia kupunguza kiwango cha sukari mwilini na presha.





                PILIPILI MANGA NA MAAJABU YAKE

Na Dk. Edger Kapagi
Pilipili manga, kwa kitaalam ‘Piper nigrum’, ni moja ya kiungo cha zamani kuliko viungo vingine na ndiyo maana kinajulikana kama mfalme wa viungo duniani.

Pilipili manga ni mbegu ndogo ndogo zenye umbo la mviringo na zenye rangi nyeusi na zingine nyeupe.

Pilipili manga imekuwa ikitumiwa na Wagiriki wa zamani na Waroma miaka mingi iliyopita.

Inasemekana asili yake ni ‘Ghats’ ya magharibi nchini India na sasa inalimwa katika sehemu nyingi za nchi za kitropiki.

Waingereza huita ‘pepper’ au ‘black pepper’ na Wahindi huita ‘kali mirch’.
Pilipili manga hutoa ladha ya muwasho mfano wa pilipili. Pia hutumika sana majumbani kama kiungo.

Pilipili manga hulimwa kwa wingi katika mikoa ya Morogoro, Tanga na visiwa vya Unguja na Pemba.

Zao hili hulimwa kama zao la biashara. Pilipili manga hustawi vizuri katika udongo wenye rutuba ya kutosha.

Lina virutubisho vingi tofauti kama protini, mafuta, nyuzinyuzi, vitamini, calcium, chuma, phosphorus, cavotene, thiamin, riboflavin na niacin.

Wapo wanaotumia kiungo hiki kikiwa kizima au katika hali ya unga (kimesagwa), inategemeana na mtumiaji anavyopendelea.

Wanawake wengi wa ukanda wa Pwani hutumia pilipili manga kuongeza ladha ya chakula kama pilau aina ya biriani.

Pia pilipili manga hutumika kama tiba kwa magonjwa mbalimbali kama kutokusagwa vizuri kwa chakula, kuondoa gesi tumboni, mafua, homa, kusahausahau, kikohozi, uhanithi ikichanganywa na lozi, maumivu ya misuli, matatizo ya meno kuuma na kuoza, harufu mbaya mdomoni, fizi kutoa damu, meno kapata ganzi na ‘pyorrhoea’.

Pilipili manga ina faida kubwa kwa mwanamke aliyejifungua hivyo ni vema uji anaokunywa uwekwe pilipili manga kidogo, kwani humsaidia kutoa uchafu uliomo kwenye kizazi.

Mwanamke anayehitaji kupata mtoto haruhusiwi kutumia kiungo hiki kwa wingi, kwani kinaweza kumsababishia kushindwa kushika ujauzito. Japo kuna vyakula vingine vilevile vinavyoweza kumsababishia kushindwa kushika ujauzito kwa urahisi.
Pia pilipili manga hutumika kwenye achali, ‘ketchups’, soseji na kukolezea vyakula mbalimbali.

Angalizo
Pilipili manga husababisha ugonjwa wa vidonda vya tumbo hasa kwa wale wanaopendelea kunywa uji uliotiwa pilipili manga kwa wingi.

Elewa kuwa utumbo ni laini sana na matumizi ya kupita kiasi huweza kusababisha vidonda vya tumbo, hivyo jali afya yako.

Hata hivyo, hukatazwi kunywa uji wenye pilipili manga ila unatakiwa kuweka kiasi kidogo sana cha kiungo hicho ili kuepusha vidonda vya tumbo.

Wanawake walioolewa wanashauriwa wapunguze matumizi ya pilipili manga. Ila, wanaweza kutumia mdalasini mzima au uliosagwa. Unga wa mdalasini unapochanganywa na asali mbichi na kutumika husaidia sana katika suala la kupata mtoto.

    

                                UMUHIMU WA VITEX MOMBASSAE
VITEX Mombassae ni mti unaoweza kukua kufikia kimo cha mita 8. Ni aina ya mimea inayopatikana sana porini, katika nchi za kitropiki. Shirika la Mbegu za Miti Tanzania (TTSA), wameuita mti wa mfudi.

Katika nchi za Afrika hupatikana Burundi, D.R. Congo, Kenya, Tanzania, Angola, Namibia, Malawi, Zambia, Zimbabwe, Mozambique na Botswana.

Mti huo hupenda udongo wa kichanga unaopitisha maji chini yake.
Nchini, mti wa mfudi una majina mbalimbali kulingana na makabila tofauti. Wazigua huuita ‘Mgobe’ na makabila mengine huuita ‘Masasati’ au ‘Nsisai’, Waingereza huuita ‘Smelly-berry Fingerleaf’ au ‘Pooraberry’.

Matunda ya mfudi hutumika sana na wachungaji wa ng’ombe na watoto. Matunda haya yana uchachu lakini yanapendwa sana na watu wengi.
Huwa yanaliwa yakiwa yameiva au kupikwa na yana vitamini C kwa wingi na virutubisho vingine.

Matunda ya mti huu ni mazuri sana kwa watu wenye maambukizi ya njia ya mkojo (U.T.I) na pia kwa akina mama wenye matatizo ya hedhi kuzidi.

Mizizi yake hutumika kutibu kisukari, ugumba (infertility) na kuzuia kutapika. Kwa wale wenye tatizo la ugumba ni vizuri wakachunguza kilichosababisha ugumba ndipo wakatumia.

Matumizi mengine ni kuwa majivu ya mti huo yanaweza kulainisha mboga wakati wa kupika.
Mti huu unatoa nguzo za kujengea, vinu na mtwangio, na miko ya kupikia n.k.
Pia tunaweza kupata kuni japo ni kuharibu mazingira na tunaweza kupata chavua kwa ajili ya asali.



 
 KUMBU KUMBU YA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE
(1922 – 1999)
Na Juma Diwani

WAKATI Taifa linaadhimisha miaka 15 kifo cha Mwasisi wa Taifa hili na Rais wa kwanza wa Tanzania, leo tunakuletea safu maalum ya historia ya Baba wa Taifa hili ili kizazi cha sasa kiweze kumjua alikuwa mtu gani na alianzia wapi mpaka alipofikwa na umauti.

Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alizaliwa mwaka 1922, katika kijiji cha Butiama, wilaya ya Musoma, mkoa wa Mara. Alikuwa moja kati ya watoto 26 wa Nyerere Burito, chifu wa kabila la Wazanaki. Alipokuwa mtoto, Nyerere alichunga mifugo ya babake na katika umri wa miaka 12, aliingia shule akitembea kilomita 30 hadi katika Shule ya Msingi ya Mwisenge, iliyoko Musoma mjini.

Baada ya kumaliza shule ya msingi, aliendelea kusoma shule ya wamishonari Wakatoliki iliyoko Tabora.
Katika umri wa miaka 20, Nyerere alibatizwa akawa Mkristo Mkatoliki hadi mwisho wa maisha yake.

Kutokana na ujasiri na nia ya kuwa mwelewa wa kila kitu ya Nyerere, mapadre wa Kanisa katoliki wakaona akili yake na nia yake nzuri ya kutaka kujifunza, wakamsaidia kusoma kozi ya ualimu katika Chuo Kikuu cha Makerere, Kampala, Uganda kuanzia mwaka 1943 hadi 1945. Akiwa katika chuo cha Makerere alianzisha tawi la Umoja wa Wanafunzi Watanganyika na pia akaamua kujihusisha na tawi la Tanganyika African Association (TAA).

Baada ya kumaliza masomo ya ualimu alirudi Tabora kufundisha Shule ya Sekondari ya Mtakatifu Maria (St.Mary´s Secondary School).
Mnamo mwaka 1949 alipata skolashipu ya kwenda kusoma kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh huko Uskoti, Uingereza kusoma Shahada ya Uzamili ya Historia na Uchumi Kwa hatua hiyo, Mwalimu alikuwa Mtanzania wa kwanza kusoma katika Chuo Kikuu cha Uingereza na mtanzania wa pili kupata shahada ya elimu ya juu nje ya Tanzania.

Aliporejea Tanganyika kutoka masomoni, Nyerere alifundisha Historia, Kingereza na Kiswahili katika shule ya St. Francis iliyo karibu na Dar es Salaam, (siku hizi Pugu Sekondari).
Mwaka 1953 alichaguliwa kuwa rais wa chama cha Tanganyika African Association (TAA), chama ambacho alikisaidia kukijenga alipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Makerere. Mwaka 1954, alikibadilisha chama cha TAA kwenda katika chama cha Tanganyika African National Union (TANU) ambacho kilikuwa cha kisiasa zaidi kuliko TAA. Ndani ya mwaka mmoja, chama cha TANU kilikuwa tayari chama cha siasa kinachoongoza Tanganyika.

Uwezo wa Mwalimu uliwashitua viongozi wa kikoloni na kumlazimisha Nyerere kuchagua kati ya siasa na kazi ya ualimu. Nyerere alisikika akisema kuwa alikuwa mwalimu kwa kuchagua na mwanasiasa kwa bahati mbaya. Aliamua kujiuzulu ualimu na kuzunguka nchini Tanganyika kuzungumza na watu wa kawaida na machifu ili kuleta muungano katika mapigano ya uhuru.

Pia alizungumza kwa niaba ya TANU katika Mkutano wa Baraza la udhamini (Trusteeship Council) ya Umoja wa Mataifa (UN) huko New York, Marekani. Uwezo wake wa kimaongezi na kuunganisha watu ulimwezesha kufanikisha Tanganyika kupata uhuru bila umwagaji wa damu. Ushirikiano mzuri aliouonesha aliyekuwa gavana wa wakati huo Richard Turnbull, ulisaidia pia kuharakisha upatikanaji wa uhuru.

Nyerere aliingia katika bunge la kikoloni mwaka 1958 na kuchaguliwa kuwa Waziri Mkuu mwaka 1960. Mwaka 1961 Tanganyika ilipata uhuru wake na Desemba 9, 1961 Nyerere alichaguliwa kuwa Waziri Mkuu wa Tanganyika huru na mwaka mmoja baadaye Nyerere alikuwa Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Tanganyika. Nyerere alikuwa kiungo muhimu katika katika muungano wa Tanganyika na Zanzibar kutengeneza Tanzania baada ya mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964, yaliyomtoa madarakani Sultani wa Zanzibar Jamshid bin Abdullah.

Hayati Mwalimu Nyerere mnamo Februari 5, 1977, aliongoza chama cha TANU katika tendo la kuungana na chama tawala cha Zanzibar ASP na kuanzisha chama kipya cha CCM (Chama cha Mapinduzi) akiwa mwenyekiti wake.

Nyerere aliendelea kuongoza Taifa hadi 1985 alipong’atuka na kumwachia nafasi Rais wa awamu ya pili Ali Hassan Mwinyi.

Aliendelea kuongoza Chama cha CCM hadi 1990 na kuwa na makini na mfuatiliaji huku akionya katika mambo kadhaa katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.

Baada ya kustaafu kazi ya ukuu wa nchi, Nyerere alikaa muda mwingi kijijini kwake alikozaliwa Butiama akilima shamba lake la mahindi. Pamoja na haya alianzisha taasisi yenye jina lake inayojulikana kama ‘Mwalimu Nyerere Foundation.’ Mwaka 1996 alionekana akiwa mpatanishi wa pande mbalimbali wa vita vya wenyewe kwa wenyewe huko Burundi.

Mwishoni mwa maisha yake, Mwalimu aliishi kama mkulima wa kawaida kijijini kwake Butiama.

Mwalimu alianza kujisikia vibaya mwezi Agosti mwaka 1999, akaanza kupata matibabu ya kila mara. Baadaye alihamishiwa katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas huko Uingereza.

Oktoba 14, 1999 aliaga dunia katika hospitali hiyo ambapo madaktari walisema kuwa alikuwa akisumbuliwa na kansa ya damu (leukemia).

Mafanikio na kasoro
Kitendo kikubwa ambacho hakisahahuliki ni kile ambacho Mwalimu alichanganya ardhi za Zanzibar na Tanganyika ambapo Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulizaliwa rasmi na hadi leo upo.


Kujenga umoja wa kitaifa na utamaduni wa Kiafrika pamoja na lugha ya Kiswahili, kushinda ubaguzi wa rangi, kutetea usalama wa taifa katika vitani dhidi nduli Idi Amin ‘Dada’ wa Uganda.

Watu walimuita ‘Mwalimu’ kwani aklikuwa ni mwanamapinduzi wa Afrika, kiongozi wa bara nzima kutokana na nia zake za kutaka kila Mwafrika kuwa huru na kuwa na amani.

Mwalimu pia alifanikiwa kutoa mchango kwa vyama vya ukombozi vya nchi za kusini ya Afrika kama Zimbabwe (ZANU), Afrika Kusini (ANC na PAC), Namibia (SWAPO), Angola (MPLA) na Msumbiji (Frelimo)

Kutofanikiwa kwake
Kitu ambacho kilimuumiza Mwalimu na kumfanya akose raha mara nyingi ni juu ya kutofanikiwa kwa nia yake ya kuanzisha siasa za Kijamaa. Siasa zake za ujamaa zilishindwa baada ya mwaka 1976.

Baada ya kuona kuwa uchumi wa Tanzania hautaweza kusimama kwa siasa za kijamaa na kutoweza kuvumilia kuendesha nchi kwa siasa ambazo yeye hakuwa muumini, Nyerere kwa maamuzi yake mwenyewe aliamua kustaafu nafasi ya urais baada ya uchaguzi wa mwaka 1985 na kumwachia usukani kwa Mwinyi aliyetawala kwa siasa za uchumi wa soko huria.

Katika hali ya kukubali ukweli, Nyerere alitamka katika tafrija ya kumwaga juu ya siasa yake kiuchumi “Nimefeli. Tukubali hivyo.”

Alikosolewa pia
Kutokana na hali hiyo na kufikia yeye kukubali kushindwa, Mwalimu Nyerere analaumiwa kwa siasa zake za kiujamaa kuwa zilichelewesha maendeleo ya kiuchumi wa Tanzania, pamoja na kwamba hata leo kuna makundi ya Watanzania kwa mtazamo wao wanazitamani siasa hizo.

Pia kuna makundi ya Waislamu wanaomtuhumu kwa kuendesha kwa siri vita dhidi ya Uislamu na upendeleo wa elimu na madaraka kwa Wakristo.

Yote kwa pamoja, Taifa la Tanzania litaendelea kumkumbuka Baba wa Taifa hili kutokana na mchango wake mkubwa katika Taifa hili, Afrika na duniani pamoja na 




          JE, WAJUA UMUHIMU WA MSHUBIRI?

Na Seif K. Oddo

Licha ya ladha yake kuwa chungu, mmea wa “Aloe Vera” una faida nyingi kiafya ukitumika kama tiba katika mwili wa binadamu.

Mmea huu umekuwa na majina tofauti tofauti kama ifuatavyo; kwa lugha ya Kiswahili mmea huu huitwa shubiri mwitu, ambapo katika makabila kadhaa mmea huu huitwa majina mbalimbali kulingana na kabila husika.

Wanyaturu huuita ‘mkankiruni’, Wagogo huuita ‘itembwe’ na wahehe huuita ‘Litembwetembwe.’

Mmea huu huwa na umbo linalofanana na mmea wa mkonge au mmea wa mnanasi, ila huu huwa mlaini zaidi.

Majani ya mmea huu yana sehemu mbili, kuna ganda la nje na majimaji ya ndani (jelly). Ganda la nje lina kemikali za kutibu na ule ute wa ndani na lina virutubisho vingi ambavyo husaidia katika kurutubisha kinga za mwili wa binadamu.

Licha ya mmea huu kuwa maarufu duniani kote, umekua ukitumika kama tiba ya magonjwa mbalimbali kwa binadamu na mifugo.

Mshubiri pori umekua ukitumika pia kwa kutengenezea vipodozi vya aina mbalimbali kwa ajili ya masuala ya urembo. 

Mmea huu hupatikana sehemu nyingi sana duniani hasa katika nchi zenye joto.

Tafiti zilizofanywa na mtandao wa ‘Mediclinic’ kuhusiana na mmea huu, zinaeleza kuwa mmea huu una uwezo wa kuchochea utengenezwaji wa tishu zenye afya katika mwili wa binadamu.

Imebainika pia kuwa mshubiri huo una uwezo mkubwa wa kufanya mfumo wa fahamu kufanya kazi vizuri na kutuliza matatizo yanayoathiri mfumo wa fahamu.

Mbali na hayo, lakini pia mshubiri “Aloe Vera” ukitumiwa kama tiba husaidia kuondoa sumu mwilini.

Mmea huu mara nyingi hutumiwa na kina baba kutibu maradhi ya ngiri (Hernia).

Kwa hakika mmea huu una maajabu mengi katika suala zima la tiba. Naweza nikadiriki kusema, mmea huu ni tunu tuliyotunukiwa wanadamu kutoka kwa Mola wetu kwa ajili ya tiba.

Sidhani kama kuna mmea wenye uwezo wa kutibu maradhi mengi namna hii kama ilivyo kwa mshubiri pori.

Haijaishia hapo pia, mshubiri hutumika katika kusaidia kujenga seli mpya katika mwili wa binadamu baada ya kupata majeraha kama vile kujikata, michubuko, majeraha ya moto na hata vidonda vya tumbo.

Aidha, husaidia matatizo ya kutopata haja kubwa, maumivu wakati wa haja kubwa na ndogo na hata husaidia kutibu matatizo ya ngozi na chunusi.

Mshubiri umekuwa ukitumika kwa wagonjwa wenye upungufu wa kinga mwilini (UKIMWI) kwa ajili ya kuongeza kinga za mwili (CD4), na imebainika mmea huu unapotumiwa vizuri, mgonjwa wa UKIMWI hujikuta katika hali nzuri.

Watu wengi wamekuwa wakitumia mmea huu kama tiba ya ugonjwa wa malaria, lakini pia mmea huu umekuwa ukichanganywa katika vipodozi mbalimbali ili kuvipa uwezo maradufu wa kutunza ngozi.

Unaweza kutumia mmea huu kwa kukata majani yake na kuyasaga kwa kutumia ‘blender’au kuyatwanga kwenye kinu, na kisha kuyachanganya na maji ya vuguvugu Chuja maji hayo na ongeza maji mpaka upate maji ya kiasi cha jagi moja.

Kunywa vikombe viwili mpaka vitatu kwa siku, kwa muda wa siku tano mpaka saba. Hii itakusaidia kuongeza kinga ya mwili wako na unaweza kurudia dozi hii kila baada ya miezi mitatu mpaka minne.

Ni vema kutumia tiba za mimea ili kuepuka kemikali zisizo za lazima katika miili yetu kiafya. Tukiangalia, pia tunaweza kuona kuwa hata baadhi ya dawa za hospitalini hutengenezwa kwa kutumia mitishamba na mimea ya asili.

Mbali na mmea wa mshubiri kutumika kama tiba kwa binadamu, mmea huu pia unaweza kutumika kama tiba kwa mifugo kama vile kuku.

Kwa mfano, ugonjwa wa vidonda vya kuku ambao kwa kitaalam huitwa ‘coccidiosis’ na ugonjwa wa mdondo ambao pia kitaalam hufahamika kama ‘Newcastle disease’ Hutibka kwa kutumia mshubiri.

Baadhi ya watu wamekuwa wakiipanda mimea hii katika bustani za maua majumbani mwao, bila ya kujua umuhimu, faida na maajabu ya mmea huu.

Ningependa kutoa wito kwa Watanzania kutopuuza matumizi ya mmea huu. Ni vema tukautumia kwa ajili ya kinga na tiba za magonjwa mbalimbli katika miili yetu.

               UKWELI KUHUSU MTOTO-3            

Nakukaribisha tena katika safu yetu ya saikolojia. Bado tunaendelea kumwangalia mtoto ambapo tuliishia kusema mtoto anapofikia miezi 46 ni sawa na miaka 3 na miezi 10. Tuliona jinsi anavyoendelea katika umri huo na umri ambao mabadiliko hutokea kwa haraka haraka. Ni wajibu wa wazazi au walezi kuwa karibu na kuwa tayari kutoa msaada pale anapokuwa tofauti na ni vizuri kumwanzishia utaratibu wa vipindi ya dini.

Mara nyingi baada ya kupitia hatua ya kupata hisia ya haja ndogo na haja kubwa, hapo kinachofuata ni hisia ya viungo vya uzazi ambapo huanza kuwa mdadisi wa kutofautisha jinsia ya kike na ya kiume.

Mpendwa msomaji kumbuka kuwa mtoto azaliwapo huwa na chachu (hormone) sawa na kadiri akuavyo, homoni huweka uwiano (balance) kulingana na umbile husika. kKwa hiyo, umri huo wa utambuzi unakuwepo wa kujijua kuwa yeye ni msichana au mvulana na huanza kujua mambo anayopaswa kuyatenda. Hapa, anatambua hata nguo na pengine kujilinganisha au kuigiza matendo yatendwayo na wakubwa na kuigiza kama baba au mama.

Huo pia ni umri wa hatari sana na ni muhimu kwa wazazi au walezi kuwa makini kwani ngono za utotoni hujitokeza kati ya umri kuanzia miaka 3 – 6. Hatua hii huitwa phallic stage na kuna baadhi ya walezi au wazazi huendelea kulala na watoto wa umri huu katika chumba kimoja au kuchanganya wa kiume na kike. Hii ni hatari kubwa.

Mfano, utamuona mtoto hatambui kitu lakini kila akionacho hukifanyia utafiti hasa kwa wale waishio mijini. Kama utazungumza na mtoto wa miaka kumi walioathirika na vitendo hivi, wengi hueleza kuwa athari waliipata katika umri huo.

Ukiwa kama mzazi, yapo mengi ya kufanya kwa watoto wapitao umri, si kwa wale tu walioathirika na vitendo hivyo, bali ni kwa watoto wote ingawa nyakati tulizonazo ni za hatari kwani ni nyakati za watu kuishi na VVU na mtoto anaweza akazaliwa na VVU na asioneshe dalili zozote katika umri huo akaingia katika hali hiyo atakuwa kwenye hatari ya kuambukizwa au kuambukiza.

Sasa tuone jinsi ya kuwasaidia watoto walio katika umri huo wanatakiwa wasivute sigara chumbani kwao, waepushe kuangalia TV (runinga) kwa muda mrefu bila kuushughulisha mwili na kusababisha nguvu ya mwili kutotumika, unene kupita kiasi, uvivu na magonjwa ya moyo na kuzidi kwa lehemu. Badala yake angeendesha baiskeli, kucheza mpira au hata kuparamia miti.


Ingawa kwa wakati huo dalili za magonjwa zinaweza zisionekane, angalia ulaji wao wasile kwa ulafi au vyakula vyenye sukari nyingi, vyakula vya nyama zaidi, ila wale milo mitatu yenye nafaka, mboga mboga na matunda.

Mzoeshe kunywa maji mengi, adabu kwa wakubwa, kushukuru, kuomba msamaha, uvumilivu, kupenda amani na kujifunza na zaidi kumheshimu Mwenyezi Mungu.

Afundishwe mazoezi, mapumziko hasa wakati wa mchana. Mzoeshe kulala mapema na kuamka mapema, kufanya ibada, usafi wa mwili na mavazi. Kuwa na fikra sawa na mtoto, jifanye kama yeye.

Cheza naye kuwa na uwe karibu naye. Mawasiliano mazuri ya mtoto hata katika umri mdogo ni muhimu.

Mpe uwezo wa kutafakari na kujiuliza yeye ni nani, maisha yana maana gani na anatakiwa kufanya nini kwa wengine na sio wengine watamfanyia nini.

Muepushe kusema uongo kwani fikra za mtoto hujengwa kutokana na akisikiacho na akionacho kwa sababu ana utambuzi na nafasi ya kujiuliza.


Mlezi kuwa mkweli kwani ukimdanganya na akajua kuwa umemdanganya hatokuamini na yeye atakuwa muongo kama mzazi mfano: mtengenezee mazingira ya adabu, usimzoeshe kuchezea pesa, mtimizie mahitaji yake kwa kumnunulia na si kumpa akanunue mwenyewe.

Chunguza michezo yake, rafiki zake, hata wazazi wao maana hao waweza kuwa maadui au chanzo cha tabia yake mbaya. Muonye huku ukimpa nafasi ya kujieleza, ruhusu hisia zake lakini asiwe mwenye maamuzi ya mwisho.

Wafundishe uchumi, kubana matumizi, asiwe mfujaji na hapa atakuwa ni mwenye kujifunza mambo mengi kwani atakuwa ameanza shule, hapo mzazi tenga muda wa kufuatilia mambo yake ya shule.

Mtoto anapokuwa na umri wa mwaka mmoja hujifunza ujamaa na ubinafsi ingawa huchukua muda kuzoea kama kushiriki michezo na wenzake ingawa huchukua muda.

Pia kuna vitu vinavyomfariji mtoto akiwa na mtu mzima mfano, anapolia, ukimbembeleza kwa kumshika nywele au kumpapasa mgongoni hujisikia raha. Fanya vile ulivyomzoesha ili akuelewe nawe umuelewe.

Mpaka hapo tumefikia tamati ya makala haya ya mtoto. Usikose wiki ijayo kuhusu vijana.


                       MAADUI WA AFYA-2

Karibu tena mpenzi msomaji wa gazeti lako pendwa la TABIBU, ni matumaini yangu kuwa ni mzima wa afya.

Kama unavyojua tumekuwa na mtiririko wa mada au somo la jinsi ya kuishi kiafya ambayo imetupelekea kuchambua mambo mengi zaidi yanayomzunguka mwanadamu katika mazingira yake ya kawaida.

Leo kutoka Miracle Food tumekuandalia hitimisho ikiwa ni mjumuisho wa yale tuliyokuwa tukiyafuatilia na tukijifunza. Karibu ujumuike nami katika makala hii.


Katika kuhitimisha somo lililokuwa likiendelea kwa wiki kadhaa zilizopita la jinsi ya kuishi kiafya, tunaona kwamba maisha ya mwanadamu yanategemea mambo mbalimbali ili kuhakikisha ana kuwa ni mwenye kuitunza afya yake na kujikinga na maradhi.

Japo wengi wakisikia mtu anazungumzia suala la afya huwa ni kama sio jambo la msingi sana lakini ukweli ni kwamba tunatumia muda mwingi sana na gharama tusizozitegemea katika kutibu maradhi ambayo yanaepukika.

Mfano kama tulivyoona, wadudu wadogo waishio majumbani ambao pengine tunawapuuza lakini wanaleta athari kubwa kwa familia zetu.


Usafi ni adui wa wadudu, mdudu hawezi kukaa mahali penye uwazi, usafi na uangalizi wa mara kwa mara. Ina maana kama utakuwa na kawaida ya kufika eneo fulani basi mdudu au mnyama atahamisha makazi. Wadudu wanaojulikana sana kuwa karibu sana na mwanadamu ni pamoja na kunguni na chawa, na hii kwa sababu wanategemea chakula pamoja na maficho kwa ajili ya makazi yao.

Tunaanza na kunguni ambao hupenda kufanya makazi yao kwenye vitanda vya mbao au vya miti vilivyotandwa kwa kili, maturubai au kamba za mimea mbalimbali.

Kunguni pia hukaa zaidi kwenye matandiko, nyufa za kuta na sakafu na kikubwa hasa anapenda kuishi katika mazingira yenye joto.

Hujipatia chakula kwa kufyonza damu za watu na baada ya kufyonza damu huacha maumivu yanayomsababisha mtu ajikune na kusababisha hata mchubuko.

Anavizia ukiwa umelala ndipo anafanya kazi hiyo. Lakini pia anaweza kusababisha homa kali.

Anauma watu mbalimbali, wazima kwa wagonjwa hivyo huweza kueneza hata magonjwa baina ya mtu na mtu. Ni hatari.

Kwa upande wa chawa, tunakuta nao wanapenda kuishi mafichoni jirani na mwanadamu. Kuna chawa wanaojificha kwenye nguo tu na wengine kwenye nywele.

Kwa wale wenye tabia ya kurundika nguo chafu ndani, watengeneza mazingira rafiki kwa ajili ya chawa.

Chawa jike hutaga hadi mayai mia mbili (200) na kuyahifadhi kwenye nywele za mwanadamu.
Hali kadhalika, chawa wa kwenye nguo hutaga mayai na kuyanatisha vizuri yasianguke kiurahisi lakini chakula chao kama kunguni, kwani nao pia hufyonza damu na kumwacha mtu akijikuna.

Ndivyo ilivyo kwa chawa na wadudu wengine wengi kama papasi, mende, mchwa, na viroboto ambao hao wana athari kubwa sana, tena hasa viroboto wa panya ambao huuma na kusambaza vijimelea vya ugonjwa wa tauni.

Kuna viroboto wa panya, viroboto wa kuku, viroboto wa mavumbini, viroboto wa maua ya miembe na wa maua ya mikorosho.


Hadi kufikia hapo mpenzi msomaji natumai kuwa utakuwa umepata mwangaza juu ya umuhimu wa kuzingatia jinsi ya kuishi kiafya. Mengi yameelezwa kwenye makala hii na pengine umeshakutana na maelezo mengi yanayoendana na usafi pamoja na afya, sasa kazi kwako kuyazingatia.

Tukutane wiki ijayo katika masomo mengine. Kama unahisi una dalili za ugonjwa ambao pengine huulewi na hujui chanzo, ni vyema kufika kwenye kituo chetu cha tiba mbadala kilichopo Kariakoo, Mtaa wa Msimbazi jengo la Klabu ya Simba ghorofa ya tatu.



JIHADHARI NA TEGUE (TAPE WORMS)

Na DK. Geoffrey  C. Lusanzu.

Tegu ambao kwa jina lingine hujulikana kama taenea solium  ni aina ya minyoo bapa yenye pingili ambayo huvamia mwili wa binadamu na kufanya maskani katika tumbo na matumbo na kukua hadi kufikia futi 20, na hatari zaidi inajitokeza pale mayai yake yanapoweza  kuingia katika mkondo wa damu na kwenda kufanya maskani katika viungo mbalimbali vya mwili.

Kuwepo kwa tegu mwilini huambatana na maumivu ya wastani na kusokotwa  tumbo, kuharisha na mwonekano wa mapingili yao katika sehemu ya msamba (anus).

Endapo mayai yake yanapata nafasi ya kupenya mwilini na kuingia katika mkondo wa damu, basi wakifanikiwa kuingia katika ubongo mtu atapatwa na kifafa (eplepsy) ambao ni mgonjwa mbaya na hatari mno.

Endapo watafanikiwa kuingia katika macho, basi mtu atapofuka macho (blindness). Takwimu za sasa zinaonesha zaidi ya watu milioni 500 ulimwenguni kote wameathirika kwa minyoo ya aina mbalimbali na tegu wakiwemo kwa kiwango cha juu mno.

Hawa tegu wapo katika makundi matatu – tegu wa Nguruwe(taenea solium), tegu wa Ng’ombe (taenea saginata) na tegu wa samaki (diphyllothrium).
Tegu  wanao athiri sana  ni wale wa nguruwe na ng’ombe.

Namna mtu anavyowapata tegu na kuhatarisha afya yake
wale walafi au wenye mazoea ya kula nyama mbichi hukumbwa na maambukizi ya tegu.

Ulaji wa nyama ya nguruwe ni hatari mno kwani minofu ya nguruwe (tissues) imeumbwa kwa makusudi kubeba vimelea wa maradhi mbalimbali na ndio maana nguruwe ni mchafu kwa asili, ameumbwa kwa kusudi hilo,na wale wanaopendelea kula mno nyama ya nguruwe hawataugua tegu tu, bali pia wataugua na maradhi mengine makali na ya kutisha mno ambayo endapo mtu anaugua na kwenda hospitali ni vigumu kuelewa  kama ugonjwa uliojitokeza una chanzo katika ulaji wa kitoweo cha nguruwe kilichokuwa kitamu sana mdomoni (very palatable).

Maradhi hayo ni pamoja na kifua kikuu, upofu,ukoma,kifafa,mchafuko mbaya wa damu,saratani,matutuo,kuharibika kwa misuli ya damu na neva,kiharusi,presha ya juu mbaya,maradhi ya akili,majipu na maradhi mengine makali ya kutisha mno.

Biblia na Korani ni vitabu vitukufu vya Mwenyezi Mungu ambaye ndiye 

Daktari mkuu  na mwumbaji wa mwili wa binadamu;Anapokataza ulaji wa nguruwe sio kwa ajili ya sababu za kidini tu, bali pia kwasababu za kiafya, na kwa hali hiyo binadamu anapaswa kuwa mtiifu na mnyenyekevu kwa mausia ya 

Mwenyezi mungu , kwani kufanya hivyo kutamwongezea heri, afya njema na maisha marefu.

Kinga na tiba asilia kwa maradhi ya tegu.

Kinga asilia: Pika nyama kwa kiwango cha joto kali mno mpaka iive kisawasawa au achana na ulaji wa nyama za wanyama na badala yake jifunze chakula mbadala ya nyama – soya, alizeti, parachichi, mikunde, karoti na karanga.

Vyakula hivi vina virutubisho asilia vinavyoshinda nyama mara dufu, navyo vikitayarishwa vizuri  ni vyakula visivyo na wadudu wa maradhi waambukizao; humpa mtu afya njema na maisha marefu ya furaha na raha.

Kumbuka kwamba ugonjwa wa tegu unaambukiza (taeniasis) uwe msafi,nawa vema kabla ya kula na baada ya matumizi ya choo.

Endapo umeathirika kwa tegu au maradhi yaliyotajwa hapo juu wasiliana na au tembelea ofisi yetu upate tiba mapema na haraka.
.




Na Dk. Fadhili Emilly

Wiki iliyopita tulikuwa tumeanza kuzungumzia juu ya matatizo ya moyo ya kuzaliwa sehemu ya kwanza, leo tunaendelea sehemu ya pili na ya mwisho.
Vilevile sababu nyingine zinazoweza kufanya mtoto azaliwe na matatizo ya moyo ni ugonjwa wa kisukari kwa mama wakati wa ujauzito.

Leo tuangalie tatizo la mtoto kuzaliwa na tundu katika kuta za juu za moyo au Atrial Septal Defect (ASD).

Wakati kijusi (fetus) kinapoendelea kukua, kuta kati ya atria mbili za moyo inayoitwa kitaalamu ‘interatrial septum’ nayo pia hukua ili kutenganisha chemba ya kulia na kushoto.

Lakini katika kipindi hiki huwa kuna tundu kati ya kuta hizo linaloitwa ‘foramen ovale’. Tundu hili ni la kawaida kwa kipindi hiki cha kijusi na husababisha damu yenye oksijeni kutoka kwenye kondo la nyuma (placenta) kutokwenda kwenye mapafu ambayo bado hayajakomaa na kuelekea sehemu nyingine za mwili hasa kichwani.

Kipande cha tishu kinachoitwa kitaalam ‘septum primum’ hufanya kazi kama valvu katika tundu hilo. Mara tu mtoto anapozaliwa, shinikizo katika mishipa ya damu ya mapafu (pulmonary circulatory system) hushuka na kusababisha tundu hilo kufunga kabisa.

Iwapo tundu hilo halitafunga wakati huu, mtoto huzaliwa akiwa na tundu katika moyo. Tundu hilo huwa halifungi kabisa kwa karibu asilimia 25 ya watu, hivyo pindi shinikizo la damu linapoongezeka katika mishipa ya damu ya mapafu kutokana na sababu mbalimbali, au kutokana na matatizo ya kikohozi cha muda mrefu, husababisha tundu la ‘foramen ovale’ kutofunga na kubakia wazi.

Tatizo hili hutokea kwa mtoto mmoja katika kila watoto 1,500 wanaozaliwa. Lakini kwa kuwa pindi mtoto anapozaliwa huwa hakuna dalili zozote za tatizo, mara nyingi huwa haligunduliki mapema hadi pale anapokua.

Zipo aina kuu 6 za tundu katika kuta za juu za moyo lakini aina ya ‘Ostium secundum’ hutokea kwa wingi, na huchangia kwa asilimia 6 hadi 10 ya magonjwa yote ya moyo ya kuzaliwa nayo.
Tatizo hilo hutokana na ukubwa wa tundu la ‘foramen ovale’ na kutokukua vyema ukuta unaoitenganisha.
 Hata hivyo, karibu asilimia 70 ya watu wenye tatizo hili huweza kufikisha miaka 40 ndipo dalili huanza kujitokeza.

Katika baadhi ya nchi zilizoendelea kama Marekani watoto wote wanaozaliwa hupimwa ili kuona kama wana tundu katika mioyo yao, na wale wanaopatikana na tatizo hilo hufanyiwa matibabu ya upasuaji na kurekebishwa tatizo hilo.

Itaendelea wiki ijayo.


UGONJWA WA MALARIA KWA MAMA MJAMZITO

Malaria ni maambukizi ya seli nyekundu za damu inayosababishwa na parasiti iitwayo Plasmodium. Plasmodiumu hawa husambazwa na mbu   aina ya Anofelesi. Mbu hutoa parasiti za malaria katika damu ya mtu aliyeambukizwa anaponyonya damu 'chakula', na kisha kupitisha parasiti anapomwuma mtu mwingine.

Parasiti hukua na kukomaa katika seli nyekundu za damu na mamilioni ya parasiti hukusanyika katika plasenta ya mjamzito.

Malaria inaweza kuwa kali zaidi kwa kina mama walio na magonjwa mengine. Malaria ni hatari zaidi kwa wajawazito kuliko watu wengine.

Dalili za malaria kwa mama mjamzito

Mama mjamzito anakuwa na dalili kama wagonjwa wengine ambao sio wajawazito. Dalili hizo ni kama vile


•Baridi (kuhisi baridi isiyo ya kawaida) na kutetemeka (vipindi vikali vya kutetemeka kwa dakika kadhaa na hudumu hadi saa 1), hii huwa dalili ya kwanza ya maambukizi
•Maumivu ya kichwa na udhaifu mara nyingi huandamana na baridi
•Joto jingi mwilini (halijoto ya juu); Joto jingi mwilini mara nyingi hufuatwa na baridi, na joto linaweza kwenda juu sana hivyo mtu anakabiliwa na deliriumu (kutokuwa katika hali sawa kiakili, kuona au kusikia mambo yasiyohalisi)
•Kutokwa na jasho joto lishukapo
•Katika baadhi ya hali zingine kuhara/kutapika kunaweza pia kushuhudiwa
•Dalili nyingine ya kawaida ni maumivu ya misuli/viungo.


Hata hivyo magonjwa mengine yanaweza kusababisha dalili kama hizi.



Wiki 12 za awali za ujauzito

Kwa kina mama wajawazito ambao hawana malaria kali dawa inayotumika kutibu malaria katika kipindi hiki ni Kwinini na Clindamycin au Kwinini pekee iwapo Clindamycin haipatikani.  Dawa hizi zikishindwa kutibu Artesunate hutumika katika matibabu kwa muda wa siku saba.


Muhula wa pili na watatu.  

Dawa mseto jamii ya Artemisin zinaweza kutumika katika vipindi hivi kutibu malaria ambayo sio kali.


Madhara ya Malaria kwa Mama mjamzito

Mjamzito aliye na malaria yuko katika hali ya kupata anemia, kuharibika kwa mimba (kutoka kwa mimba pekee yake kabla ya wiki 24 za ujauzito), kuzaa mapema, kupata mtoto mdogo zaidi, kuzaa mtoto aliyekufa (mtoto kuzaliwa akiwa amekufa baada ya wiki 24 za ujauzito) au kufa yeye mwenyewe (kifo cha mama).


Kukinga na Malaria
Kukinga malaria inapaswa kuwa wajibu wa mtu binafsi na jamii.Mama mjamzito afanye kila awezalo kuepuka kuumwa na mbu.Hata hivyo matumizi ya vyandarua pamoja na kuangamiza mazalia ya mbu hupunguza kuenea kwa ugonjwa wa Kukinga malaria inapaswa kuwa wajibu wa mtu binafsi na jamii


FAHAMU FAIDA ZA BEETROOT (Beta vulgaris)

Na Dk. Edger Kapagi

Namshukuru mwenyezi mungu kwa kunipa afya njema.

Mwaka huu nilipata fursa ya kuhudhuria maonesho ya Siku ya Wakulima maarufu kama nane nane katika viwanja vya John Mwakangale Nyanda za juu kusini na nilijifunza kuwa watu wengi hawafahamu wa faida za vyakula tunavyo kula. 

Na katika maonesho yote niliyoyaona nilivutiwa na banda moja tu la Halmashauri  ya Mbeya vijijini.

Halmashauri hii ilibandika maelezo ya kila mmea waliopanda na faida zake na watu wengi hawakujua faida za beetroot na hii ndiyo sababu iliyonifanya niandike makala hii ili kuwaelimisha watu juu ya faida za mmea huo.

Asili ya beetroot ni Ulaya na imetumiwa na Wagiriki na Waroma kwa miaka mingi iliyopita na hivi sasa inalimwa ulimwenguni kote. Kinachotumiwa ni majani na mizizi.

Juisi ya beetroot ni moja ya juisi bora kwa afya ya binadamu beetroot ni chanzo kikuu cha sukari ya asili, calcium, sodium, potassium, phosphorus, sulphur, chloline,iodine,choline, vitamin B1,B2, Niacine,B6 na C.

Juisi ya beetroot ni nzuri sana kwa figo na gall bladder. Madini ya chuma yaliyomo kwenye beetroot yanafaa kurutubisha Anaemia.

Juisi ya beetroot ikichanganywa na karoti na tango ni nzuri sana kwa wenye upungufu wa nguvu za kiume, mawe ya kwenye figo,gall bladder, ini na matatizo ya tezi dume (Prostate troubles) na kutengeneza damu mwilini.

Beetroot ni kizuia saratani (tumour_inhibiting component). Juisi ya beetroot ni nzuri kwa kichefuchefu na kutapika kuna tokana na acidity, homa ya manjano, hepatitis, kuharisha, kutosagika kwa chakula na Dysentery.

Juisi hii ichanganywe na juisi ya ndimu ndio inakuwa bora zaidi.

Juisi ya Beetroot ikichanganywa na kijiko cha asali na ikanywewa asubuhi kabda ya kufungua kinywa ni nzuri kwa vidonda vya tumbo aina ya gastric ulcer.

Juisi ya majani ya beetroot ikichanganywa na juisi ya ndimu ni nzuri kwa homa ya manjano na vidonda vya tumbo (gastric ulcer)kama inanywewa mara moja kila siku.

Ulaji wa kila siku wa beetroot huzuia ugonjwa wa kukosa choo na piles.

Juisi ya beetroot ikitumiwa mara kwa mara utaepukana na magonjwa ya hypertension, arteriosclerosis na matatizo ya moyo.

Wazungu na watu wa Asia hutumia beetroot kama mboga, salad, juisi na supu.

Watanzania tuanze kutumia beetroot kwa faida ya afya zetu.


MUUJIZA WA ASPARAGUS OFFICINALIS
Na Edger Kapagi
Mmea huu umekuwa ukilimwa na kustawi sehemu mbalimbali huko Ulaya sehemu zenye udongo wa kichanga.

Pia hustawi vizuri katika nchi za India, China, Taiwan, Afrika na Malaysia. Jina la kitaalam huitwa ‘Chlorophy tumborivianum.’ Wahindu huuita shatawar au sootmuli. Kwa Waingereza, mmea huo huuita Asparagus.  Majani yake huliwa na mizizi yake hutumika kama dawa.

Nchini Tanzania, hupatikana kwa wingi mikoa ya Iringa, Njombe, Dar es Salaam na Arusha. Kwenye asparagus officinalis, kuna protini, mafuta kidogo, nyuzinyuzi, kabohaidreti, kalishi, phosphorus, magnesium, chuma, vitamin A, vitamin B-complex na vitamin C/

Mizizi (rhizome) yake hufaa sana kwa wenye matatizo ya moyo uliotanuka na udhaifu wa moyo,. Mizizi hiyo ikichanganywa na asali ni chakula kinachofaa sana kwa watu wenye magonjwa ya moyo.

Mizizi ya asparagus imekuwa ikitumiwa katika dawa za Yunani huko India kwa miaka mingi ambapo huamsha tendo la ndoa. Asparagus ina mchango mkubwa wa kuchochea homoni za kijinsia hivyo huamsha na kuongeza hisia za nguvu za kike na kiume.

Kwa sasa, mmea huo umekuwa na mahitaji makubwa huko Mashariki ya Kati na Ulaya.

Dawa hiyo huuzwa kwa kutumia jina la ‘Safedmusli’ na huuzwa ghali.

Vile vile, huongeza ukubwa na huweza kutanua misuli mirefu na unene wa utupu wa mwanaume kama unatumiwa mara kwa mara na kupunguza matatizo ya uhanithi (impotency).

Uwepo wa saponins na alkaloids zinazoongeza nguvu za uzazi pia umefanya mmea huu kuwa maarufu katika jamii mbalimbali.

Tahadhari;
Watu walio na matatizo ya mawe kwenye figo, cystitis, kisukari, nephritis au jongo (gout) wasitumie mpaka watibu matatizo waliyo nayo.



Na Dk. Fadhili Emily

Leo tutajadili baadhi ya matatizo ya moyo ya kuzaliwa kwa jina la kitaalam huitwa Congenital Heart Disease.

Magonjwa ya moyo ya kuzaliwa yapo mengi, kuanzia yale yanayosababishwa na matatizo madogo madogo ambayo kwa kawaida huwa hayaoneshi dalili au kuathiri maisha ya kawaida ya mtu, hadi yale makubwa yanayohitaji kutibiwa kwa haraka.

Mara nyingi matatizo ya moyo ya kuzaliwa ni yale yanayozuia mtiririko wa damu katika moyo au kwenye mishipa ya damu, au kusababisha damu ipite njia nyingine isiyokuwa ya kawaida kwenye moyo.

Matatizo mengine ya moyo ya kuzaliwa lakini yasiyotokea sana ni pale baadhi ya chemba za moyo zinapokosekana au badala ya kuwepo chemba mbili, mtoto huzaliwa na chemba moja ya ventricle au wakati mwingine upande wa kulia au wa kushoto wa moyo huwa haujaumbika kwa ukamilifu, hali ambayo kitaalam huitwa hypoplastic heart.

Miongoni mwa sababu zinazosababisha watoto kuzaliwa na matatizo ya moyo ni pamoja na mmoja kati ya wazazi kuwa na tatizo la moyo la kuzaliwa. Iwapo mama alikuwa na tatizo la moyo la kuzaliwa kuna uwezekano wa asilimia 2.5 hadi 18 wa kuzaa mtoto mwenye tatizo la moyo pia. Iwapo baba alikuwa na tatizo la moyo la kuzaliwa, uwezekano wa kuzaliwa mtoto mwenye tatizo la moyo ni kuanzia asilimia 1.5 hadi 3.

Si kawaida mtoto zaidi ya mmoja kuzaliwa na tatizo la moyo katika familia moja. Kuna uwezekano mtoto aliyeko tumboni wakati moyo unapoumbwa akapatwa na maambukizi ya maradhi kama vile ‘rubella’, au kuathiriwa na dawa anazotumia mama wakati wa ujauzito au sumu kama vile ‘lithium’ na hata pombe.

Yote hayo yanaweza kusababisha mtoto azaliwe na matatizo ya moyo.
Pia baadhi ya matatizo ya kijenetiki huambatana na matatizo kadhaa ya moyo ya kuzaliwa. Matatizo hayo ya jenetiki kitaalam huitwa Down’s Syndrome, Digeorge syndrome na Turners Syndrome.

Jambo lingine linaloweza kusababisha mtoto azaliwe na matatizo ya moyoni ni pale mama anapokuwa na tatizo la kijenetiki linalojulikana kama Phenylketonuria (PKU). Hali hiyo hutokea wakati mwili unaposhindwa kuyeyusha sehemu ya protini inayoitwa phenylalanine (Phe).

Phenylalanine kwa kawaida hupatikana katika kila chakula lakini kiwango chake kinapokuwa juu mwilini huweza kuharibu ubongo na kusababisha mtindio wa ubongo. Baadhi ya wajawazito hupata tatizo hilo ambalo huzidisha uwezekano wa mtoto kuzaliwa akiwa na matatizo ya moyo na ya ubongo pia.

Itaendelea wiki ijayo.
STAFELI NI TIBA YA SARATANI

Na Kennedy Chaya
Stafeli ni tunda la chanikiwiti ambalo linastawi zaidi katika ukanda wakitropiki. Mti wa tunda hilo ni mfupi wa wastani na Wabrazili wanauita ‘graviola’ na Waingereza wanauta ‘soursop’. Hapa Tanzani stafeli linajulikana kwa jina jingine la topetope.

Kwa Waingereza, tunda hili ni kubwa lenye uchachu wa kati na utamu mwingi. Ndani yake kuna maganda yenye weupe kama sufi na limesheheni juisi.
Nchini Tanzania, unaweza kupata mtopetope au mstafeli katika mikoa ya Rukwa, Mbeya, Iringa, na Ruvuma. Mikoa mingine ni Morogoro, Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro, Bukoba, Arusha, Tanga na sehemu na mikoa mengine ambapo unaelezwa kuwa unapatikana

Tunda la stafeli linadhaniwa kutibu magonjwa kadhaa, ikiwamo saratani kwa ubora wa karibu mara 10,000 ya matibabu ya kawaida yanayopatikana kwenye vituo vya afya, utafiti umebaini. Wataalam wanasema kuwa utafiti zaidi unahitajika kudhibitisha hili.

Utafiti huo uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dawa cha Purdue nchini Marekani, umeeleza kuwa mbali na kutibu saratani, tunda hilo pia lina uwezo wa kutibu matatizo ya msongo na mfadhaiko.

“Uzuri wa stafeli ni kwamba lina uwezo wa kuangamiza chembehai zenye saratani pasipo kusababisha madhara katika mwili wa binadamu kama zinavyofanya dawa zingine za ugonjwa huo au mionzi,” imesema sehemu ya utafiti huo uliochapishwa kwa mara ya kwanza katika Jarida la Kemia na Madawa la nchini Marekani, mwaka 2010.

Taasisi ya utafiti wa Saratani ya Nchini Uingereza (NIR) ilifanya utafiti wa kwanza kuhusu maajabu ya stafeli mwaka 1976.

Katika utafiti huo, ilibainika kuwa majani, mizizi na tunda la stafeli, vina uwezo wa kutibu saratani, lakini matokeo ya utafiti huo hayakutangazwa kwa umma kwa hofu ya kuua viwanda vya dawa za saratani.

Inaelezwa kuwa kirutubisho kilichopo katika stafeli kinatumia jina la kibiashara la ‘Triamazon’ na kimepigwa marufuku kutumika nchini Uingereza na Marekani kutokana na uwezo wake mkubwa wa kitiba.

Utafiti mwingine uliofanywa na Chuo Kikuu cha Kikatoliki nchini Korea na kuchapishwa katika jarida la Bidhaa Asilia ulibaini kuwa stafeli lina uwezo wa kuponya saratani ya tumbo.



Utafiti wa chuo hicho ulienda mbali na kusema kuwa tunda hilo linaweza kulenga seli za saratani tu, bila kushambulia seli muhimu za mwili kama ambavyo tiba ya mionzi ifanyavyo.

Tunda la stafeli mabalo jina lake la kisayansi ni ‘Annona Muricata’, ambacho ndicho chenye uwezo wa kupigana na maradhi ya saratani.
Imeelezwa kuwa stafeli lina uwezo wa kutibu aina 12 za saratani ikiwemo ya matiti, kongosho, mapafu na ya kibofu cha mkojo.

Pamoja na kutibu saratani, tunda hilo pia huweza kutibu vimelea, shinikizo la damu, msongo wa mawazo, matatizo ya mfumo wa fahamu na sukari.

Utafiti huo unaonesha kuwa kirutubisho kimegwacho katika tunda hilo kina uwezo wa asilimia kubwa kupambana na saratani bila kumuacha mgonjwa na madhara kama kusikia kichefuchefu, kutapika, kupungua uzito na kunyonyoka nywele.

Aidha, stafeli huweza kuupa mwili kinga na nguvu bila madhara yasababishwayo na dawa nyingine. Tangu mwaka 1976, tunda hilo liliendelea kufanyiwa utafiti katika maabara binafsi zaidi ya 20 duniani.


KUTOKA VICTORIA THERAPIES
MADHARA YATOKANAYO NA KUJICHUA (MASTUBATION)  -1

Na Dk. Emmanuel
Mastubation   ni ile hali ya mwanaume kujichua sehemu zake za siri (uume) kwa kutumia mkono hadi manii yake yatoke kwa lengo la kupunguza hisia zilizotokana na hamu ya kushiriki tendo la ndoa.

Kujichua imeonekana ni tatizo katika jamii mbalimbali kwani mwanaume anapotokea kukosa kiasi (moderation) kunapelekea yeye kuwa na matatizo mbalimbali.

Kwa upande mwingine kuna faida kimwili pamoja na kiakili kwani mtu anayejichua kwa kiasi anafaidika kama ifuatavyo:

1.  Kujichua kiasi kunasaidia mtu aliyechagua kutojiingiza katika tendo la ngono kabla ya ndoa.

2. Kwa mtu anayejichua na kufika kileleni vizuri, kuna kemikali ambazo zinatolewa na ubongo kama dopamine, endorphine, selotonin, melatonin na oxtocin, homoni zinazofanya kazi mwilini kama ‘neurotransmitters’ ambazo faida zake ni:

- zinamfanya mtu anakua na hali nzuri (mood)
- zinasaidia kuchochea kupata usingizi mzuri
- kusaidia uwezo wa muda wote kutunza kumbukumbu
- muda wote anajisikia furaha
- zinaongeza kinga za mwili                                                                 
- kuongeza uwezo wa kuweka maungo bora
- kuongeza uwezo wa maamuzi katika utokaji wa manii
- kupunguza msongo wa mawazo
- ni njia salama kwani mfanyaji hawezi kupata magonjwa ya ngono kama UKIMWI, kaswende, gono n.k

Tukumbuke pia kuwa kila kitu kizuri kikitumika kupita kiasi kinaleta madhara kwa upande wa pili, na madhara yake ni makubwa zaidi kuliko faida. Madhara yake ni kama yafuatayo:

         - Upungufu wa nguvu za kiume, kwa maana mtu anapojichua anaumiza misuli ya uume, hivyo                        hupelekea kusinyaa hata kwa mishipa ya damu na kutofanya kazi vizuri, kutofanya kazi kwa mishipa ya fahamu (nerves) ambapo kunapelekea kushindwa kusimamisha uume vizuri, au uume kusimama legelege, kufika kileleni mapema na kushindwa kururdia tendo la ndoa baada kumaliza (kufika kileleni).

         - Uchovu, muda mwingi mwili unakuwa dhaifu. Hii inatokana na uzalishaji mwingi endorphine ambayo inafanya kazi kama ‘sedative’ au dawa ya usingizi ambayo inapelekea misuli ya mwili kusinyaa muda wote.

 - Kupoteza kumbukumbu au kutokua na uwezo wa kutunza kumbukumbu. Hii ni kwa sababu ya utolewaji wa mara kwa mara na kiasi kikubwa cha dopamine, selotonin, melatonin, ambazo zinafanya kazi mbalimbali pamoja na kusaidia kuendesha mifumo ya ubongo inayofanya kazi za dharura (quick response) au ‘sympathetic nervous system’ ambao ni mfumo wa ubongo unaofanya kazi ya mwili ukiwa umetulia (relaxed) na kwa utaratibu. 

Hivyo mtu anapojichua mara kwa mara anasababisha hizo kemikali zitolewe kwa wingi hatimaye kuathiri hiyo mifumo pamoja na medula ambayo ni sehemu ya ubongo inayotunza kumbukumbu.

-       Kushiundwa kuwa na  uwezo wa kuweka mawazo karibu na katika tukio linalofanyika kwa muda huo (lose concentration) kwa sababu mtu anapojichua mara kwa mara anapelekea uzalishwaji mwingi wa  adrenaline, dopamine, seletonin zinazoathiri ‘amydala’ ambayo ni sehemu ya ubongo inayofanya kazi ya ‘attention na concentration’ na hatimaye mtu anakuwa hana uwezo wa kuweka mawazo yake karibu kwa maana anafanya kitu lakini mawazo yake hayapo kwenye kile kitu anachokifanya (kupoteza umakini).

-       Kushindwa kufanya kazi nzito kwa kutumia akili au mwili kwa sababu misuli inakuwa imesinyaa muda wote.

-       Kupoteza uwezo wa kuona. Hii ni kwa sababu ya utokwaji wa dopamine, selotonin, adrenaline kwa wingi. 
Hizi homoni kwa muda mwingi zinatumika kwa mfumo wa ubongo unaoshughulika na mambo ya dharura (sympathetic response) ambapo wakati huo mboni ya jicho inakua inatanuka ili kuongeza uwezo wa kuona ili kupambana na hali ya hatari.   
Mfano, mtu anapokuwa na hasira au ghafla anakutana na simba, mwilini huwa kuna mabadiliko yanatokea ili kupambana na hatari. Njia mojawapo ni kuongezeka kwa kasi ya mapigo ya moyo, kupumua haraka haraka, joto kupanda, ambapo mabadiliko hayo yanasababishwa na hizo na homoni, hivyo basi kutokana na kuzalishwa mara kwa mara adrenaline, dopamine na selotonin kunapelekea hiyo mboni ya jicho kutanuka kupita kiasi na hatimaye kupoteza uwezo wa kuona.

-       Kunyonyoka kwa nywele au kuwa na kipara. Hii ni kwa sababu mtu anapojichua mara kwa mara anasababisha uzalishwaji mwingi wa ‘dehydrotestosterone hormone’ (DHT) ambayo inaathiri ukuaji au utoaji wa nywele.

-       Mastubation wakati mwingine inaweza kuwa kama ulevi hadi kunamfanya mtu anayejichua kupunguza uthamani wa tendo la ndoa hatimaye asiwe na uwezo /hamu ya kushiriki tendo la ndoa na mwanamke na hata akishiriki hawezi akawa na msisimko kama anaoupata akiwa anajichua.

-       Maumivu ya mgongo/ kimo na misuli ni dalili au matokeo ya                       kujichua.

USHAURI
Epuka kujichua kwa faida ya  afya ya ubongo na mifumo yote ya mwili. Hivyo kama unasumbuliwa na dalili nilizozitaja hapo juu na ulishawahi kujichua wahi haraka hospitali. Au pia kwa ajili ya matibabu na ushauri zaidi tembelea VICTORIA THERAPIES iliyopo Mtoni Kijichi kwani hiki ndio mkombozi wa matatizo yote ya kiume hususan upungufu wa nguvu za kiume na mengineyo yanayohusu mfumo wa uzazi wa mwanaume kwa ujumla.

    
     



 KUTOKA MIRACLE FOOD

MAADUI WA AFYA


Karibu mpenzi msomaji wa Gazeti la TABIBU katika safu ya Miracle Food Clinic & Counseling. Leo tunaenda kuangalia panya anavyohatarisha afya zetu. 

Panya ni mnyama anayeguguna vitu na vyakula, anaishi porini na anaweza kuishi katika nyumba zetu. Panya jike huzaa watoto 10 au zaidi kwa mara moja. 

Chakula chake hasa ni nafaka, lakini hula pia aina nyingine za vyakula akivipata.

Panya wakiingia katika nyumba huishi mahali palipo jificha na penye giza giza. 

Mathalani katika dari, ghala au kwenye stoo ya chakula. Pia katika makabati, ndani ya majiko yaliyotengenezwa mithili ya kabati, kwa mfano majiko makubwa ya umeme au gesi, vilevile huishi katika sehemu za friji. 


Madhara yanayoletwa na panya

Panya ni wanyama wa kuepuka sana kwa sababu hueneza magonjwa hasa ugonjwa wa tauni ambao ni hatari sana.


Mtu akiumwa na viroboto vilivyomuuma panya mwenye tauni naye anaweza kupatwa na ugonjwa wa tauni.



Nyumba hupata ubovu kutokana na mashimo yanayochimbwa na panya katika sakafu na kuta.


Mashimo haya yanaweza kuwapatia maskani wadudu wengine na vilevile kuingiza katika nyumba viumbe wa hatari kama vile nyoka.



Panya ni waharibifu sana wa vyakula na vitu vingine vilivyomo katika nyumba.

Wao hula na huharibu kiasi kikubwa cha chakula katika muda mfupi tu.

Huguguna na hutoboa toboa vitabu, magazeti, nguo, mablanketi, magodoro, viatu, sabuni, waya za redio na vitu vingine.Huuma watu wanapokuwa wamelala usingizi.

Panya hupenda kuwauma katika viganja vya nyayo, hasa ikiwa sehemu hizi hazikusafishwa vizuri, zinatoa harufu mbaya au zina vidonda visivyofunikwa. 

Wakiuma sehemu zenye vidonda, huongeza maumivu na kuvifanya viwe vibaya zaidi.

Kuzuia na kuangamiza panya

·      Fanya ukaguzi wa kutosha katika sehemu zote za nyumba mara kwa mara pamoja na kuziba haraka mashimo na nyufa katika sakafu, kuta na dari.
·      Panga vizuri ghala ya chakula. Hakikisha kuwa ghala ni safi wakati wote na inapata hewa na mwangaza wa kutosha.
·      Funika vyakula, pia tunza vyakula katika kabati lenye wavu, friji kama unalona, katika vyombo vinavyofaa vyenye mfuniko, kwa mfano madebe, makopo, vibuyu na vyungu.
·      Funga kwenye karatasi masalio ya chakula yasiyofaa halafu yatupe katika pipa lenye mfuniko au yafukie vyema.
·      Funika vizuri pipa la takataka ili panya wasiingie mara kwa mara, choma moto, fukia au zika takataka.
·      Fuga paka hodari anayeweza kula au kuua panya.
·      Tumia mitego kuwanasa panya, lakini angalia mambo yafuatayo
-       Tega mitego hasa wakati wa usiku kwa sababu panya hujitokeza zaidi wakati huu.
-       Weka kwenye mtego kipande kidogo tu cha chakula kinachoweza kuwavutia panya, mathalani kilichobaki cha samaki au nyama
-       Waarifu watu wanaoishi pamoja nawe kuhusu mtego, wajulishe mahali ulipoweka iliwatahadhari wasije wakaugusa au kuukanyaga kwa bahati mbaya.
Mpenzi msomaji natumaini hadi kufikia hapo utakuwa umepata kujua japo kwa ufupi jinsi panya anavyohatarisha afya zetu na jinsi ya kumdhibiti. Kama unasumbuliwa na panya nyumbani ni vyema kufika kwenye kituo chetu cha tiba mbadala kujipatia sumu ya panya na isiyo na madhara kwa binadamu. 



Na wale wa matibabu utamuona daktari na kupima, ni gharama nafuu. Kwa wale wa mikoani, kuna punguzo la bei za dawa. Karibuni wote.


Kwa mawasiliano na huduma nyingine za kiafya, naushauri fika Miracle food clinic & Counseling - Kariakoo Mtaa wa Msimbazi jengo la Klabu ya Simba ghorofa ya tatu au piga simu namba:




       TAMBUA UMUHIMU WA MAJI KWA AFYA YAKO

Na Seif Oddo
Maji ni kitu muhimu sana katika maisha ya viumbe hai wote, hakuna kiumbe hai wa aina yoyote anayeweza akaishi bila ya kuhitaji maji.

Katika mwili wa binadamu, maji yanachukua nafasi kubwa zaidi katika kuimarisha afya. Wataalam wa afya wanaeleza ya kwamba mwili wa binadamu umejengwa kwa asilimia 65 na 75 za maji kwa kutegemea unene wa mtu, ambapo watu wembamba wana kiasi kikubwa zaidi cha maji kuliko watu wenye miili minene.

Imekua ni jambo la kawaida kwa watu wengi kutotilia maanani suala la unywaji wa maji, ambapo wengi wetu tumekua tukinywa maji pale tu, tunapohisi kiu au pale tunapokula chakula.

Hii ni kutokana na kutofahamu umuhimu wa maji katika miili yetu, au kama tunafahamu basi tunapuuza.

Wataalam wa afya wanatueleza kwamba, mapafu ya binadamu yanahitaji vikombe viwili hadi vinne vya maji kila siku ili kuweza kufanya kazi kiufasaha zaidi.

Kunywa maji ya kutosha kila siku, husaidia kupunguza uwezekano wa kutokea mawe katika figo na hata kulainisha viungo na kuzuia mafua.

Wanaendelea kueleza asilimia 60 ya uzito wa mwili wa binadamu ni maji na mfumo wa mwili hutegemea maji kwa kiasi kikubwa ili kuweza kufanya kazi.

Inaelezwa kuwa maji husaidia katika kurahisisha mfumo wa mmeng’enyo wa chakula, na pia maji husaidia kuboresha afya ya ngozi ambapo huboresha tishu za ngozi na kuongeza unyevu kwenye ngozi na kuonekena mng’avu.

Hata hivyo maji pia husaidia ubongo kuwa na uwezo mzuri wa kufanya kazi na kumfanya mtu awe na uwezo mzuri wa kufukiri.

Wataalam wanaeleza kuwa, maji husaidia katika kupunguza uwezekano wa kupata magonjwa kama ya ini, mafua na mawe kwenye figo.

Imeelezwa ya kuwa matumizi ya maji ya kutosha huweza kumuepusha mtu kupata tatizo la choo kigumu yaani constipation.

Maji husaidia kuepusha tatizo la kubanwa na misuli na kuepusha msuguano wa 
viungo vya mwili.

Wataalam wa tiba wanaendelea kueleza umuhimu wa maji katika mwili wa binadamu ambapo wanaeleza ya kwamba, maji husaidia kuondoa uchovu na pia huchochea shughuli za kimetaboliki mwilini, pamoja na kupunguza uzito mwilini.

Ongezeko la ufanisi wa figo na ini katika mwili wa binadamu kutokana na kunywa maji kwa wingi husaidia kuondoa mafuta ya ziada mwilini.

Tafiti mbalimbali za kisayansi zilizofanywa zimethibitisha umuhimu wa maji katika mwili wa binadamu.

Chama cha madaktari nchini Japani kimethibitisha kwamba maji yana uwezo wa kuponya kwa asilimia 100 endapo yatatumika kwa kuzingatia taratibu za kitabibu.

Miili yetu hupoteza maji kila siku kwa kutokwa na jasho, kukojoa na hata kutoa pumzi nje yaani exhaling na harakati za tumbo, ambapo kitaalam hujulikana kama bowel movement.

Ili mwili uweze kufanya kazi vizuri zaidi, unahitaji kurudisha maji hayo.

Hivyo tunashauri kunywa maji ya kutosha kila siku ili kuimarisha afya zetu.

Wataalam walio wengi wanakubaliana kwamba, binadamu anatakiwa kunywa vikombe vinane vya maji kwa siku.

Pia baadhi ya wataalam wanashauri kwamba wanaume wanywe maji kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko wanawake, kutokana na tofauti za miili yao.

Wataalam wa afya wanashauri tunywe kikombe kimoja cha maji dakika 30 kabla ya mlo, hii husaidia kupata choo vizuri.

Pia inashauriwa kunywa kikombe kimoja cha maji kabla ya kwenda kuoga, kwani husaidia kupunguza shinikizo la damu.

Vile vile inashauriwa kunywa kikombe kimoja cha maji kabla ya kwenda kulala kwani husaidia kuzuia shinikizo la moyo.

Hivyo basi maji ni muhimu katika mwili wa binadamu tukajijengea mazoea ya kunywa maji ya kutosha mara kwa mara ili kuimarisha afya zetu na kuepuka magonjwa mbalimbali.

MARADHI YA KUUMA NA KUVIMBA MAUNGIO (ARTHRITIS) - 4

Dk. Geoffrey C. Lusanzu
Mpenzi msomaji, hii ni makala ya nne tukielezea elimu ya afya juu ya kujikinga na maradhi makali, sugu na korofi ya baridi yabisi (arthritis).

Maradhi haya yanazidi kushika kasi katika jamii ya binadamu na kuwaacha wengi wakiwa walemavu na wengine kufariki dunia, lakini endapo hukupata sehemu ya kwanza hadi ya tatu ya mada hii, tafadhali hakikisha unafanya juhudi kupata nakala zilizopita ili ujipatie elimu hii ya thamani kubwa kwa kutembelea www.tabibumedia.blogspot.com.

Tuisemeje hali ya kuuma na kuvimba maungio ya viungo?
Ni kuvimba kwa ungio moja au zaidi mwilini kunakosababishwa zaidi na mharibiko wa misuli midogo ya damu pamoja na kudorora kazi kwa neva katika eneo lenye matatizo.

Dalili
Eneo lililoathirika huwa jekundu, maumivu makali au wastani, joto kwa ndani mithili ya kutokeza moto, kuvimba, ugumu wa eneo linaloathirika au kukakamaa, kujisikia mchovu wakati wote, kuchoma mithili ya sindano, homa, kutoinama kirahisi, kukunja au kukunjua viungo kwa shida pamoja na ganzi.

Magonjwa yapi yanaitwa baridi yabisi?
Mharibiko wa ungio (osteoarthritis), kuvimba na kuuma maunganio (rheumatism), kuvimba na kuuma maungio mengi na kwa ukali na usugu mwingi (rheumatoid arthritis), kuvimba na kuuma vifuko vya maji katika maungio (bursitis), kuvimba na kuuma katika uti wa mgongo (ankylosing spondylitis), kuvimba na kuuma katika kiungo kimoja au zaidi (infective arthritis), homa ya baridi yabisi (rheumatic fever) na gauti (gouty arthritis)

Nini chanzo cha maradhi haya?
Ni sumu za ‘uric acid’ zilizozidi na kuuzinga mwili. Sumu hizi huletwa na ulaji mwingi wa vyakula vya nyama. Pia wadudu waambukizao maradhi kama vile virusi, mfumo wa kinga ya mwili kujivuruga wenyewe na urithishwaji ni visababishi muhimu.
Hata hivyo, kwa wale wanaotumia pombe, tumbaku, chai, kahawa, bangi watakumbwa na maradhi haya.

Nini humkera zaidi mgonjwa wa baridi yabisi?
Uvimbe na maumivu wakati fulani huambatana na kuchomachoma mithili ya pini au sindano na ganzi pamoja na kuwaka moto, hali ambayo huashiria kwamba uhai una hitilafu kubwa katika eneo linaloumwa na hali hii humkatisha mgonjwa tamaa ya kupona.
·      Je mtoto mdogo anaweza kuugua baridi yabisi?
Ndiyo, inawezekana kabisa kwani maradhi haya hutegemea uambukizo wa wadudu wa maradhi, mfumo wa kinga unaojivuruga (autoimmune response) na urithishwaji.

·      Mganga anawezaje kuutibu ugonjwa huu?
Kwa kujua dalili au kupima damu katika maabara kwa kutumia vipimo vya kisasa kama vile ESR, RF test, ANA test, X-Ray, CTI, MRI na vingine vingi huweza kubaini maradhi ya baridi yabisi.
Atakupa dawa mbalimbali na kukupa ushauri madhubuti pamoja na kufanya mazoezi ya viungo vya mwili.

·      Baridi yabisi inaathirije maisha ya mtu?
Mtu asipotibiwa huwa mlemavu na pengine viungo vyote vya mwili kama vile figo, ini na moyo hudhurika na kudorora kazi. Mtu hawezi kuzalisha mali, na mwisho kufariki mapema.

Kama umeathirika tayari na baridi yabisi wahi uende hospitali ukatibiwe mapema. Waweza kuwasiliana nasi pia ukatibiwa kwa kutumia dawa asilia zenye nguvu isiyo na mpinzani. Mungu ni mwema sana, tuonane tena juma lijalo!


1 comment:

  1. Kwa zaidi ya miaka 13 ya ndoa sikuweza kuzaa, naendelea kuharibika hata nikipata mimba, madaktari wote hawakuweza kunisaidia, hadi dada yangu akanielekeza kwa Dr DAWN, ambaye alinisaidia nikapata ujauzito na sasa hivi kuwa na mtoto mzuri wa kike,
    Anasaidia pia marafiki zangu wengi niliowaelekeza, Dr DAWN ni baraka kwa kila mtu anayewasiliana naye,
    *Kama unataka kupata mimba.
    *Ukitaka kuacha kuharibika kwa mimba.
    *Ukitaka kumrudisha mpenzi wako.
    *Kama unataka mume/mkeo arudishwe.
    *Kama unataka kurejesha mali yako iliyoibiwa au Pesa.
    *Ukitaka kutibu aina yoyote ya ugonjwa,
    Wasiliana naye kwa WhatsApp: +2349046229159

    ReplyDelete