Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

Wednesday, August 27, 2014

Ona jinsi mzee huyu anavyoteswa na maradhi ya kibofu

Na Kenneth Maganga
Kushoto ni mwandishi wa TABIBU  akizungumza na Mzee Maulid alipomtembelea nyumbani kwake Mbagala Kongoe (Picha na mwandishi wetu)
  • ·      Kwa sasa anakojoa kupitia mirija

  • ·      Awaomba Watanzania kumsaidia na ikiwezekana aonane na JK


Mzee Maulid Kakonda mkazi wa Mbagala Kokongoe jijini Dar es Salaam amekuwa akiteseka na maradhi ya kibofu cha mkojo tangu mwaka 2012 na kupelekea kuishi na maumivu makali katika maisha yake tangu kukubwa na maradhi hayo.

Akizungumza na TABIBU hivi karibuni, Mzee Maulid anasema kuwa maradhi hayo yalianza kumsumbua mwaka 2012, ambapo alijikuta akianza kupata haja ndogo kidogo sana (mkojo), pamoja na maumivu makali na baadaye alishindwa kabisa kupata mkojo.

“Kwenye siku mbili tatu niliona mkojo unatoka kidogo sana na baadaye ukabana zaidi na kuacha kabisa kutoka,” alisema mzee Maulid.

Baada ya hali hiyo mzee Maulid anasema alilazimika kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili, ambapo madaktari waligundua alikuwa anasumbuliwa na tatizo la uvimbe kwenye kibofu na kupelekea kufanyiwa upasuaji na kuwekewa mirija miwili ambayo ndio inamsadia katika kutoa haja ndogo kwa sasa.

Kutokana na hali hiyo mzee huyo anasema kwa sasa kila baada ya wiki mbili huwa anakwenda hospitali kubadilisha mirija, ambapo anasema mara nyingi anapobadilishwa mirija hiyo hupatwa na maumivu makali ambayo mara nyingi humsababishia homa kali.

Mzee Maulid, anasema tangu alipoanza kusumbuliwa na maradhi hayo amekuwa akipatiwa matibabu bure, baada ya kupata msamaha wa matibabu, ambao aliupata kutokana na juhudi za Serikali yake ya mtaa, lakini kwa sasa anasema muda wa msamaha huo umekwisha, hivyo anahitajika kutoa pesa ili kuweza kuendelea na matibabu zaidi hususani upasuaji mwingine wa pili.

Hapo awali kabla ya maradhi hayo mzee Maulid, anasema alikuwa akipata ridhiki kupitia kuchukua magazeti yaliyokwisha somwa katika ofisi mbalimbali, kisha kuyauza kwa wamiliki wa maduka, ambayo hutumika kufungia bidhaa mbalimbali. Lakini kwa sasa kutokana na maradhi yake hayo amekuwa akishindwa kufanya shughuli hizo hivyo kupelekea maisha ya familia yake yenye jumla ya watu 6 kuwa katika hali ngumu zaidi.

“Maisha yangu bado ni ya shida kwa sasa, kwa sababu hapa nilipo bado sijajua lini nitapata uzima, lakini naamini kwa uwezo wa mwenyezi Mungu madaktari watanifanyia huduma,” alisema Mzee Maulid.

Mbali na maradhi hayo mzee Maulid pia anatatizo la ulemavu, ambapo anasema ulemavu huo aliupata kupitia kwa waganga wa jadi, baada ya kukupwa na ganzi mwilini, tatizo lililompelekea kwenda kwa waganga wa jadi ambako alikuwa akipatiwa matibabu ya tatizo hilo kwa njia ya kuchua.

“Mimi nilizaliwa mzima kabisa, lakini matatizo haya ya miguu yametokana na waganga wa jadi, ambao walikuwa wakinichua sana pindi nilipokuwa nikisumbuliwa na ganzi mwilini, lakini kumbe walikuwa wananichua kwa nguvu nyingi sana na mwishowe nilijikuta nikiwa katika hali hii unayoniona nayo,” alisema Mzee Maulid.  

Pamoja na hayo, mzee huyo amewaomba Watanzani kumsaidia ili aweze kuendelea na matibabu yake, lakini pia ameomba kusaidiwa kutokana na hali ngumu ya maisha yake anayoipitia kwa sasa yeye pamoja na familia yake.

Hata hivyo, Mzee Maulid alisema kuwa angefarijika sana endapo angefanikiwa kuonana na Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa lengo la kumuelezea matatizo aliyonayo hususani juu ya maradhi yake hayo.

“Unamuona kijana yule aliyeungua moto, alisaidiwa sana na Mheshimiwa Rais Jakaya, hivyo na mimi nilikuwa namuomba mheshimiwa rais nimuone kwa hali na mali, ili nimuelezee shida niliyoipata na matatizo yangu ana kwa ana ili na mimi anisaidie maana najua tatizo langu hili anaweza kunisaidia,” alisema Mzee Maulid kwa kusisitiza sana. 
Naye Abdala Mpanjinji ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Mzinga kata ya Tuangoma wilaya ya Temeke amekiri kumfahamu mzee Maulid mtaani hapo na namna anavyokabiliwa na matatizo ya maradhi yake hayo.

Hata hivyo, Mpanjinji amesema wamekuwa wakimsaidia kwa namna mbalimbali ikiwa ni pamoja na masuala ya matibabu yake, ambapo walimsaidia kumuandikia barua kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, ambapo barua hiyo ilimsaidia kupatiwa matibabu bure tangu mwaka 2012.

Aidha, Mpanjinji ameongeza kuwa kwa sababu muda wa msamaha wa matibabu umeshakwisha kwa sasa, lakini bado wao wapo tayari kumuandalia barua nyingine itakayomuwezesha kumsaidia kuendelea kupata matibabu kwa msamaha.

Madaktari wanasemaje kuhusiana na matatizo ya kibofu cha mkojo?
Daktari kiongozi wa Hospitali ya Amana Dk. Gilbert Ngua aliliambia TABIBU kuwa ugonjwa huu huweza kusababishwa na mambo mengi na kitaalamu huitwa ‘bladder Outlet Obstruction’ (BOO).

Dk. Ngua anasema miongoni mwa mambo yanayoweza kupelekea matatizo katika kibofu cha mkojo ni pamoja na kuvimba kwa tezi dume (prostate hyperplasia), mawe kwenye mfuko wa mkojo (bladder stones), magonjwa ya zinaa hususani kisonono, makovu (urethral scars), vichocheo (hormones) pamoja na umri nk.

Aidha, Dk. Ngua alizataja dalili za tatizo hili kuwa ni pamoja na kupatwa na maumivu chini ya kitovu, kukojoa mara kwa mara hasa usiku, kujisikia kibofu kujaa muda wote, tumbo kujaa hasa chini ya kitovu, kupata shida wakati wa kukojoa (hesitancy), kujikojolea (incontinence), sambamba na mkojo kukosa nguvu (weak stream).

Hata hivyo, daktari anashauri watu kwenda hospitali kupima ili kujua chanzo cha tatizo, huku akisema tiba ya tatizo hilo hutegemea chanzo na mara nyingine upasuaji huweza kuhitajika.

Wataalam wa tiba asilia wanasemaje?
Dk.Geoffrey Lusanzu, ambaye ni Mkurugenzi wa kituo cha Tanamerec Herbal Clinic kilichopo Kabanga wilayani Kasulu mkoani Kigoma naye anasema sababu huwa ni matatizo ya tezi dume, ambapo tezi hizo huweza kuharibika ama kwa kukonda au kupanuka.

Dk. Lusanzu anasema hali ya kupanuka hufanya tezi dume kulalia mirija ya mkojo na hivyo kuifanya mirija hiyo ipinde na kusababisha mkojo kushindwa kupita kirahisi.

Hata hivyo, naye anasema kuwa kwa kawaida hali hiyo husababishwa na maambukizo ya wadudu wa maradhi au hali ya umri wa uzee hususani kuanzia miaka 50 na kuendele. Huku akiongeza kuwa tiba asilia zina nguvu kubwa ya kutibu tatizo hilo kwa muda wa wiki 4 tu.

Kwa habari kama hizi na nyingine nyingi hakikisha hukosi nakala yako ya TABIBU kila siku ya Alhamisi kwa shilingi 500/= tu



No comments:

Post a Comment