Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

Sunday, August 10, 2014

Imarisha afya yako kwa kufanya mazoezi






Na Seif K. Oddo
 Ni ukweli usiopingika, japokuwa tuliowengi hatufahamu ya kwamba magonjwa mengi yanayosumbua miili yetu tunajitengenezea au kujisababishia sisi wenyewe. Miili yetu imeumbwa ili iweze kutumika katika kiwango fulani, hivyo kuitumia chini au juu ya kiwango hicho husababisha magonjwa mbalimbali.
Maendeleo ya teknolojia yameleta starehe au raha na kurahisisha maisha kwa kiasi kikubwa, ila nyuma ya maendeleo haya ya teknolojia yamebeba athari za kiafya katika miili yetu bila ya sisi kufahamu. Kwa mfano watu wengi kwa sasa wamekuwa wakipenda kutumia magari katika matembezi, tena hata kwa umbali mdogo, watu wengi hupenda kuketi kwa muda mrefu majumbani wakiangalia tamthilia katika televisheni zao. Walio wengi wanapenda kufanya kazi zisizotumia nguvu hata kidogo, pia watu wengi hupenda kutumia lifti kupanda katika majengo marefu wanapokwenda maofisini mwao.
 Mfumo huu wa maisha ya aina hii ndio hasa unaopelekea tushindwe kutumia miili yetu ipasavyo pamoja na virutubisho tunavyokula katika vyakula mbalimbali. Miili yetu haihitaji kiasi kikubwa cha virutubishi hivi na visipopunguzwa hurundikana na kuwa sumu ambayo husababisha magonjwa mbalimbali kama vile kisukari, saratani na magonjwa mengineyo.
Hapo ndipo umuhimu wa kufanya mazoezi unapochukua nafasi kubwa katika kulinda na kuimarisha afya ya binadamu. Mazoezi ni tiba na pia ni kinga ya mwili wa binadamu dhidi ya magonjwa mbalimbali.Kupitia mazoezi, tunaweza kupunguza mafuta na kuondoa baadhi ya sumu ndani ya miili yetu na hata kupunguza uzito wa mwili ambao pia huwa ni kikwazo kiafya.
Hivyo basi tunashauriwa kufanya mazoezi mara kwa mara ili kuimarisha afya za miili yetu. Ni vyema mtu akatenga muda maalum kwa ajili ya kufanya mazoezi, kama unavyotenga muda maalum kwa ajili ya kula. Inashauriwa mbali na kutenga muda huu, pia ni lazima kuheshimu kwa kufuata ratiba ya mazoezi uliojipangia ili kufikia lengo. Kuna baadhi ya sehemu za miili yetu hazitibiki kwa dawa au kwa upasuaji isipokuwa kwa mazoezi pekee. Hivyo basi mazoezi ni kitu muhimu sana kuliko watu wengi wanavyodhani.
Kwa mujibu wa tafiti mbalimbali, imebainika kuwa kwa kufanya mazoezi unawezesha mwili kutumia virutubisho ipasavyo, kwani hakutokuwa na kinachohifadhiwa ama kubaki mwilini kinyume na matakwa ya mwili.
Sio lazima mtu ufanye mazoezi magumu sana, kuna aina tofauti za mazoezi ambayo unaweza kuyatumia kwa afya. Kwa mfano kutembea umbali mrefu, kukimbia taratibu kwa umbali mrefu, kuendesha baiskeli na mazoezi ya viungo.
Wanasayansi wa Chuo Kikuu cha Karolinska nchini Sweden, wamebainisha katika tafiti zao kwamba kutembea kwa kawaida kwa muda wa saa moja kwa siku, kwa muda wa siku tano kunaweza kushusha kiwango cha sukari kwa wagonjwa wa kisukari na kufikia kiwango cha kawaida kwa asilimia zaidi ya sabini.
Utafiti uliofanywa na wanasayansi kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi za Tiba cha Muhimbili, hapa nchini umeonesha kwamba watu wenye tabia ya kufanya mazoezi mara kwa mara, wana kinga zaidi ya kutopata maradhi ya kisukari na moyo ukilinganisha na wale wasiofanya mazoezi kabisa.
Mbali na hayo, tafiti zimeonesha jamii zinazoishi vijijini na kujishughulisha na kilimo pamoja na ulaji wa vyakula vya asili ikiwemo kujishughulisha na shughuli zinazotumia nguvu, zimekuwa na kiasi kidogo sana cha magonjwa ya kisukari, moyo na saratani ikilinganishwa na jamii zinazoishi maisha tunayoyaita ya kisasa, ambapo watu hawapendi kabisa kusumbua miili yao.
Ikumbukwe kwamba mazoezi yanatambuliwa kama dawa katika nchi mbalimbali, mazoezi yana uwezo mkubwa wa kuzuia kisukari, ugonjwa wa moyo, unene wa kupindukia, saratani, magonjwa ya viungo, msongo wa mawazo na magonjwa ya mfumo wa homoni. Hakika kinga ni bora kuliko tiba, gharama ndogo itakayokugharimu kwa kufanya mazoezi, sio sawa na gharama kubwa itakayokukumba kwa kutibu magonjwa ambayo ungeweza kuyadhibiti kwa kufanya mazoezi tu.
Ni ngumu kuamini kwamba wakati mwingine unaweza kujiepusha na kifo kwa kufanya mazoezi, kwani watu wengi hupoteza maisha kwa kushambuliwa na magonjwa ambayo wangeweza kuyadhibiti na kuyaepuka kwa kufanya mazoezi, hapo unaweza kuona ni kwa kiasi gani mazoezi yalivyo muhimu katika maisha yako.
Baadhi ya watu wanadhani mazoezi ni kwa ajili ya kutengeneza maumbo mazuri ya miili tu, wengine wanaamini mazoezi ni kwa ajili ya watu wanene tu. Ukweli ni kwamba, mbali na kutengeza maumbo mazuri ya miili, lakini pia hata watu wasio na miili minene wanapaswa kufanya mazoezi kwani mazoezi, yanaboresha afya na kusaidia kuzuia magonjwa hatari mwilini.
Kwa wale wanaopenda kutumia lifti kuelekea katika ofisi zao, ni vyema wakatumia ngazi badala ya lifti au tumia lifti hadi ghorofa chache  kabla ya kufika katika ghorofa uendayo, kisha shuka kutoka katika lifti na umalizie kwa kupanda ngazi mbaka ufike unapoelekea.
Na kwa wale wanaotumia usafiri mara kwa mara, ni vyema ukatafuta sehemu ya umbali wa kiasi uliegesha gari lako, kisha tembea kwa miguu hadi ofisini kwako na endapo unafanya kazi zisizotumia nguvu, jitahidi kwa kiasi fulani kufanya kazi ukiwa umesimama, ili kuepuka kukaa kwa muda mrefu, ambapo itakusaidia kuepuka matatizo ya uti wa mgongo, na badala yake simama na tembeatembea hapo ofisini.
Wataalam wa masuala ya afya wanashauri kunywa maji ya kutosha baada ya kufanya mazoezi, kwa wale wanopenda kufanya mazoezi magumu kama vile kunyanyua vyuma vizito, inashauriwa kupata ushauri wa daktari kabla ya kuanza mazoezi hayo.
Nakushauri ndugu Mtanzania msomaji wa blog hii ya TABIBU, kama hujaanza mazoezi anza sasa na ukumbuke mwili wako ni kitu chenye thamani kubwa kuliko kitu kingine chochote hapa duniani.Hivyo basi, kuulinda mwili wako ni jukumu lako. Epuka kujibweteka na uanze kuupa mwili mazoezi ya kutosha ili kujenga afya bora. Kumbuka, mazoezi ni tiba.

No comments:

Post a Comment