Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

Friday, December 19, 2014

Fahamu kuhusu ugonjwa wa Kaswende - 1

Na Abdallah Juma

Ugonjwa wa kaswende ni ugonjwa wa zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya ‘Treponema pallidum’.

Ugonjwa huu ni kati ya magonjwa ya zinaa yanayoongoza kwa kusababisha madhara mengi.


Maambukizi ya kaswende wakati wa ujauzito huleta madhara mengi sana kama vile kujifungua kiumbe ambacho kimeshakufa, mtoto kuathirika na ugonjwa huu wakati wa kuzaliwa, mtoto kupata matatizo wakati wa ukuaji wake, degedege na kuongezeka kwa vifo vya watoto wachanga. 

Ugonjwa wa kaswende huathiri zaidi ya mimba milioni moja duniani kote kila mwaka na kuchangia theluthi mbili ya vifo vya watoto wanaozaliwa wakiwa tayari wameshakufa katika nchi za maeneo ya chini ya Jangwa la Sahara. Asilimia 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende huishia watoto kufariki wakati wa kuzaliwa.

Pia asilimia nyingine 30 ya mimba zinazoathiriwa na kaswende husababisha watoto wanaozaliwa na ugonjwa huu kupata matatizo ya ukuaji, degedege na kuongezeka vifo vya watoto kwa asilimia 50.

Kwa mfano, Taasisi ya kudhibiti Ugonjwa wa UKIMWI nchini Tanzania (Tanzania National AIDS Control Programme) au NACP katika ripoti yake ya utafiti uliofanywa chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii nchini ilitangaza kuwa, maambukizi yote ya kaswende wakati wa ujauzito Tanzania bara kati ya mwaka 2003 hadi 2004 yaliongezeka kwa wastani wa asilimia 6.7 kwa ujumla, kuanzia mkoani Kilimanjaro ambako maambukizi yalikuwa ya asilimia 0.4 hadi mkoani Tabora ambako yalikuwa ya asilimia 32.

Magonjwa ya UKIMWI na kaswende mara nyingi huambatana pamoja ambapo pia ugonjwa wa zinaa wa kaswende huongeza uwezekano wa mtu kupata UKIMWI.

Je, ugonjwa wa kaswende huambukizwa kwa njia gani?
Kama tulivyosema awali, kaswende husababishwa na bakteria aina ya Treponema pallidum.
Miongoni mwa njia za ugonjwa huu nipamoja na
·      Kupitia kujamiiana bila kutumia kinga au ngono zembe na mtu aliyeambukizwa kaswende.
·      Mama aliyepata ugonjwa wa kaswende wakati wa ujauzito anaweza kumuambukiza mtoto wake wakati wa ujauzito.
·       Kuambukizwa kupitia michibuko au mipasuko kwenye ngozi wakati wa kujamiiana au wakati mwingine pale mtu anapogusana na mtu mwenye kaswende ikiwa wote wawili wana mipasuko kwenye sehemu mbalimbali za ngozi zao.

Sio rahisi mtu kutambua kama ana michibuko au la kwenye ngozi kwani mingine huwa midogo sana isipokuwa ile inayoweza kuonekana kwa macho, lakini huweza kuwa njia ya maambukizo.

Dalili na viashiria vya tatizo hili
Dalili na viashiria vya ugonjwa wa kaswende hutegemea aina ya ugonjwa wa kaswende wenyewe.
Kuna aina tano za ugonjwa wa kaswende ambazo ni;
§  Ugonjwa wa kaswende wa awali (Primary syphilis)
§  Ugonjwa wa kaswende wa pili (Secondary syphillis)
§  Kaswende iliyojificha (Latent syphilis)

§  Kaswende ya baadaye (Tertiary syphilis). Itaendelea.............

No comments:

Post a Comment