Tabibu Tv

Tabibu Tv

EBOLA BBC NEWS

Thursday, July 24, 2014

MAUMIVU YA TUMBO YA MARA KWA MARA KWA WANAWAKE WOTE DUNIANI

Wanawake wanaosumbuliwa na maumivu ya tumbo chini ya kitovu mara kwa mara hupata athari nyingi baadaye endapo kama hawatagundua chanzo cha maumivu hayo.

Katika tumbo la mwanamke kuna mfumo wa kawaida wa tumbo ambao ni tumbo la chakula na mfuko wa haja kubwa, kuna kibofu cha mkojo na mfumo wa mkojo.
Pia kuna mfumo wa uzazi ambao ndiyo tunaozungumzia leo kwa undani.

Mfumo wa chakula una matatizo yake mengi ambayo huambatana na kichefuchefu na kufunga choo, mfumo wa mkojo nao una shida nyingi tu ambazo ni maambukizi au ‘UTI’ au Yutiai ambayo huambatana pia na maumivu katika njia ya mkojo.
Matatizo ya mfumo wa uzazi huambatana na dalili mbili, mojawapo ni ile ya kutokwa na uchafu ukeni.

Chanzo cha tatizo
Maumivu ya mara kwa mara ya tumbo kwa wanawake yanahusiana zaidi na mfumo wa uzazi. Maumivu haya yanaweza kuwa maambukizi katika mfumo wa uzazi ambayo huathiri kuta za ndani za uzazi, maambukizi yanasambaa hadi katika mirija ya uzazi hali iitwayo ‘Salpingitis’ na huweza kusababisha mirija kujaa maji ‘Hydrosalpinx ’ au kujaa usaha ‘Pyosalpinx’.

Maambukizi pia husambaa hadi katika vifuko vya mayai ‘Oophoritis’.
Maambukizi pia huwa ukeni na kitaalamu huitwa ‘Vaginitis’ na hushambulia kuta za uke, yakifika katika mlango wa shingo ya kizazi huitwa ‘Cervicitis’.

Pamoja na kushambulia ndani ya uke na shingo ya kizazi, pia hushambulia nje kabisa ya uke ambapo mwanamke hulalamika muwasho nje ya uke kwenye midomo au mashavu ya uke na hata kutokwa vipele.

Dalili za tatizo
Mwanamke mwenye tatizo ukeni hulalamika muwasho ukeni na kutokwa na uchafu ambao mara nyingi huwa na harufu kama shombo la samaki. Pia hulalamika maumivu wakati wa tendo la ndoa.

Mwanamke ambaye maambukizi yamefika katika mlango wa shingo ya kizazi hupatwa na maumivu wakati wa tendo la ndoa na wakati mwingine hutokwa na damu wakati wa kujisafisha huona damu kidogo au kama hakuna damu atahisi mdomo wa kizazi umevimba na kushika kitu kama kigololi ndani ya uke.

Mwanamke pia hulalamika kama kuna kitu kinasukumwa wakati wa tendo la ndoa.
Maumivu ndani ya kizazi hasa katika kuta za ndani hupatwa na maumivu baada ya tendo la ndoa, vilevile hupatwa na maumivu chini ya tumbo muda wote yaani kila siku na kumnyima raha. Maumivu wakati wa hedhi na kutokwa na damu nzito nyeusi na wakati mwingine hutoa harufu.

Maumivu yakiwa katika mirija ya uzazi husambaa chini ya tumbo kulia na kushoto, maumivu pia huwa ya muda mrefu na hali hii humfanya mgonjwa apate haja kubwa kwa shida.
Maambukizi katika vifuko vya mayai husababisha siku za hedhi zivurugike na ziwe hazina mpangilio maalum, huathiri upevushaji na uzalishaji wa mayai hivyo kushindwa kupata ujauzito.

VYAKULA VYA KUEPUKA KWA MJAMZITO

Ili mtoto azaliwe akiwa na afya njema pamoja na akili timamu, akiwa tumboni lazima alishwe lishe bora na mlo sahihi. Mwenye jukumu la kutoa lishe bora na sahihi kwa kiumbe kilichomo tumboni ni mama. Anatakiwa kujua aina ya vyakula anavyopaswa kula. Vivyo hivyo, anatakiwa kujua aina ya vyakula vya kuviepuka.



Katika makala ya leo, tunaangalia orodha ya vyakula vilivyokatazwa. Mama mja mzito haruhusiwi kuvila vyakula vifuatavyo kwa faida ya kiumbe kilichomo tumboni na kwa faida yake mwenyewe:

NYAMA MBICHI
Epuka kula samaki au nyama mbichi au iliyopikwa lakini haikuiva vizuri. Utajiepusha na uwezekano wa kula bakteria na vijidudu vingine hatari kwa afya ya mtoto tumboni. Mjamzito anapokula nyama, anatakiwa kuhakikisha imeiva sawasawa.

‘SOSEJI’ NA ‘SANDWICHI’
Mjamzito haruhusiwi kula ‘soseji’, ‘sandwichi’ za nyama na vyakula vingine vilivyotengenezwa kwa nyama. Inaaminika kuwa nyama zinazoandaliwa kwa ajili ya kutengenezea vyakula kama hivyo, huwa vimewekewa vihifadhi vyakula (preservatives) ambavyo vinaweza visiwe vizuri kwa afya ya mtoto.

SAMAKI WENYE ZEBAKI (MERCURY)
Wajawazito wamekatazwa kula samaki wenye kiasi kingi cha madini ya zebaki. Ulaji wa zebaji kwa wajawazito umehusishwa na uzaaji wa watoto taahira. Mfano wa samaki hao ni pamoja na Papa, Chuchunge na dagaa wakubwa.

MAYAI MABICHI
Ulaji wa mayai mabichi au vyakula vilivyochanganywa na mayai mabichi, mjamzito haruhusiwi kuvila. Kuna baadhi ya ‘Ice Cream’ na ‘mayonaizi’ hutengenezwa kwa kuchanganywa na mayai mabichi. Mjamzito amekatazwa kuvila vyakula hivyo.

MAINI
Maini yana kiwango kikubwa cha madini aina ya chuma. Hata hivyo, yana kiasi kikubwa cha Vitamin A ambacho huweza kuwa na madhara kwa mtoto kikizidi.

MAZIWA MABICHI
Maziwa mabichi huweza kuwa na bakteria ajulikanae kama ‘Listeria’, ambaye huweza kusababisha kuharibika kwa mimba. Unapokunywa maziwa, hakikisha yamechemshwa au kama ni ya paketi hakikisha ni yale yaliyoandikwa ‘Pasteurized’ na siyo ‘Unpasteurized’.

KAFEINI (CAFFEINE)
Ingawa baadhi ya utafiti unaonesha kuwa unywaji wa kiasi kidogo cha kafeini hauna madhara, lakini kuna utafiti mwingine unaonesha kuwa unywaji wa kafeini una uhusiano na kuharibika kwa mimba. Kafeini ni aina ya kirutubisho kinachopatikana ndani ya kahawa.

Iwapo mjamzito atakunywa kahawa, basi anywe kiasi kidogo sana kisichozidi kikombe kimoja kwa siku. Kwa kawaida kahawa hukausha maji mwilini, hivyo unywaji wake husaidia kukauka maji mwilini ambayo ni muhimu sana kwa mjamzito.

Utafiti mwingine unaonesha kuwa kafeini inahusishwa pia na uharibikaji wa mimba, uzaaji wa watoto ‘njiti’ na watoto wenye uzito mdogo. Ni vizuri kunywa maji ya kutosha, maziwa na juisi na kuepuka kunywa vinywaji vyenye kahawa.

POMBE
Hakuna ushahidi unaothibitisha kuwa unywaji wa pombe kiasi kidogo wakati wa ujauzito hauna madhara, kwa maana hiyo matumizi ya pombe hayaruhusiwi kabisa wakati wa ujauzito, hata kama ni kidogo.
Unywaji wa pombe wakati wa ujauzito huweza kuathiri ukuaji mzuri wa mtoto. Kutegemeana na kiasi atakachokunywa mjamzito, pombe inaweza kumsababishia mtoto ugonjwa hatari utokanao na pombe (Fetal Alcohol Syndrome).